05 September 2013

NYOTA WA AIRTEL RISING STARS KWENDA NIGERIA



Na Mwandishi Wetu
TIMU za wavulana na wasichana wenye umri chini ya miaka 17, ambazo zitaiwakilisha Tanzania kwenye michuano ya kimataifa ya Airtel Rising Stars, zinaingia kambini jijini Dar es Salaam kesho kufanya maandalizi ya mwisho kabla ya kwenda nchini Nigeria kushiriki michuano hiyo.

Akizungumza Dar es Salaam jana Ofisa Uhusiano wa Airtel Tanzania, Jane Matinde alisema wachezaji hao chipukizi watashughulikia kukamilisha hati zao za kusafiria kati ya leo na kesho."Kwa upande wetu kila kitu kimekamilika kwa ajili ya safari kwenda kwenye mashindano hayo ya kimataifa, ambayo yatashirikisha timu kutoka sehemu mbalimbali barani Afrika," alisema.
Jane alisema jumla ya wavulana na wasichana 32 walifuzu kwenda kuiwakilisha Tanzania kwenye mashindano hayo, baada ya kuonesha uwezo mkubwa wa kucheza mpira wa miguu, wakati wa fainali za Taifa za Airtel Rising Stars, zilizofanyika Dar es Salaam Juni.Alisema mashindano hayo ya kimataifa yanafanyika kwa mara ya pili mwaka huu, yakiwa na lengo la kutoa fursa zaidi kwa wachezaji chipukizi kuendeleza vipaji vyao.
Kwa mara ya kwanza mashindano ya kimataifa ya Airtel Rising Stars yalifanyika jijini Nairobi mwaka jana, ambapo Tanzania iliwakilishwa na timu ya wavulana pekee ambayo hata hivyo ilitolewa hatua za awali, huku timu ya Nigeria ikitawazwa kuwa mabingwa."Kulingana na kiwango cha kuridhisha cha wachezaji waliochaguliwa mwaka huu, nina imani kwamba timu zetu za Tanzania wasichana na wavulana zina nafasi nzuri ya kufanya vizuri," alisema.
Alisema Airtel imeanzisha mashindano hayo ya vijana barani Afrika kwa nia ya kusaidia upatikanaji wa vijana wenye vipaji vya soka kuanzia ngazi ya chini hadi taifa.Ofisa huyo alisema Airtel Rising Stars, inatoa fursa kwa vijana kudhihirisha uwezo wao kwa makocha wa taifa na kimataifa na kuweza kujiendeleza zaidi kisoka.
Airtel Rising Stars ni moja ya matukio ya kisoka ambayo yapo kwenye kalenda ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Huanzia katika hatua ya usajili ikifuatiwa na mechi za mtoano, ili kupata wachezaji nyota wa kuunda timu za mikoa ambazo huchuana katika ngazi ya taifa

No comments:

Post a Comment