18 September 2013

PONDA AKWAMA



  • MAHAKAMA YAKATAA OMI LAKE,ARUDI SEGEREA
  • AFIKISHWA MAHAKAMANI CHINI YA ULINZI MKALI


 Mshtakiwa Shekhe Ponda Issa Ponda akiwasili katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoani Morogoro chini ya ulinzi mkali wa askari wa Jeshi la Magereza.
 Baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu waliofurika kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoani Morogoro,wakiwa wamekaa chini na wengine kusimama baada ya kuzuiwa kuingia ndani ya chumba cha mahakama. Kulia ni askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), mkoani Morogoro akilinda usalama.

 Shekhe Ponda akiwa katika chumba cha Mahakama ya Hakumu Mkazi mkoani Morogoro chini ya ulinzi wa askari Magereza.
 Na Ramadhan Libenanga,Morogoro

Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoani Morogoro, jana imekataa ombi la dhamana ambalo liliwasilishwa na wakili upande wa utetezi, Bw. Juma Nassoro katika kesi ambayo inamkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini,Shekhe Ponda Issa Ponda.


 Katika kesi hiyo, Shekhe Ponda anakabiliwa na mashtaka matatu likiwemo la uchochezi anayodaiwa kuyafanya Agosti 10 mwaka huu, eneo la Kiwanja cha Ndege, Morogoro.Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Bw. Richard Kabate, alisema mahakama haiwezi kumpa dhamana Shekhe Ponda kutokana na mambo matatu mbali ya kwamba dhamana ni haki ya mshtakiwa kikatiba.

Mambo hayo ni pamoja na hati iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), iliyozuia mahakama hiyo isitoe dhamana kwa mshtakiwa.Bw. Kabate alisema, pia mshtakiwa amekiuka amri ya kutotenda kosa lolote katika kipindi cha mwaka mmoja na kutotoka nje ya Dar es Salaam ambayo ilitolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Msingi wa kesi

Shekhe Ponda alifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Agosti 19 mwaka huu, kwa usafiri wa helikopta akitokea mahabusu ya Gereza la Segerea, Dar es Salaam.Mahakama hiyo ilifurika umati wa watu wakiwemo wafuasi wake ambapo Jeshi la Polisi, liliimarisha ulinzi katika eneo lote la mahakama hadi kesi hiyo ilipoahirishwa.

Baada ya Shekhe Ponda kutoka mahakamani na kuona umati mkubwa wa watu, aliwapungia mkono na kujibu salamu hiyo kwa kusema "Takbriir, Allahu Akbar" (Mungu Mkubwa).Wakili wa Serikali, Benard Kongola, alisema Shekhe Ponda alialikwa kutoa maelezo machache kwenye Kongamano la Eid lililoandaliwa na Umoja wa Wahadhiri mkoani humo na kutamka maneno ambayo ni kosa kisheria.

"Ndugu Waislamu, msikubali uundwaji wa kamati za ulinzi na usalama za misikiti kwani kamati hizo zimeundwa na Baraza la Waislamu Tanzania (BAKWATA), ambao ni vibaraka wa CCM na Serikali, kama watajitokeza kwenu na kujitambulisha, fungeni milango na madirisha muwapige"

Alidai kwa maneno hayo, Shekhe Ponda alivunja masharti ya mahakama ya kifungo cha nje kilichotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ya Mei 9 mwaka huu na kutakiwa ahubiri amani.

Katika shtaka la pili, Shekhe Ponda anadaiwa kuwashawishi wafuasi wake kutenda kosa la jinai kwa kuwaambia, "Serikali ilipeleka jeshi mkoani Mtwara ili kushughulikia suala la vurugu iliyotokana na gesi kwa kuwaua, kuwabaka, kuwatesa wananchi kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake  ni Waislamu.

"Serikali haikufanya hivyo kwa wananchi wa Loliondo ambao walikataa Mwarabu asipatiwe kipande cha ardhi ya uwindaji baada ya kudai ni mali yao kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni Wakristo."Shtaka la tatu ni kudaiwa kutamka maneno yaliyoumiza imani ya watu wengine kama yalivyo katika shtaka la pili.

Baada ya kusoma mashtaka hayo, Bw. Kongola alisema walikuwa na mashahidi 15 na vielelezo vitatu ambavyo ni DVD mbili na kibali kilichotolewa na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Morogoro (OCD), Agosti mosi mwaka huu cha kongamano hilo na hati ya hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Kisutu, Mei 9 mwaka huu.

Sheikh Ponda aliyakana mashtaka hayo ambapo Wakili wa utetezi, Bw. Nassor aliwasilisha ombi la dhamana kwa mteja akisema mashtaka hayo kisheria yana dhamana.Pia Bw. Nassoro aliwasilisha ombi la kupatiwa hati yenye maelezo ya mlalamikaji ambaye  ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kudai kuwa, kutokana na upelelezi upande wa mashtaka kukamilika, wanahitaji maelezo hayo ili waweze kuandaa utetezi.

Bw. Kongola aliiomba Mahakama kutompa dhamana mshtakiwa kutokana na cheti kilichotolewa na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), kupinga dhamana ya mshtakiwa huyo kwa ajili ya usalama wa nchi.Hakimu Kabate aliahirisha kesi hiyo na kudai Septemba 17 mwaka huu, Mahakama hiyo ingetia uamuzi kama mshtakiwa atapewa dhamana au la.

1 comment:

  1. Aliosema sk,Ponda yote ni sahihi hakuna hata en moja la unfiki, Ila kwa sababu madia zote ni zenu basi fanyeni mtakalo ,lkn mkae mkijua iko cku halali na harmu, ukweli na uongo na hizo fitna zenu zina mwisho wake, ALLAH KARIM

    ReplyDelete