06 September 2013

MWALUSAKO: NIPO TAYARI KUONDOKA YANGA



 Na Amina Athumani
KATIBU Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako amesema ataondoka katika klabu hiyo, endapo uongozi wake utamtaka afanye hivyo.Mwalusako ambaye alikaimu nafasi ya Katibu Mkuu kwa muda mrefu sasa, alisema yupo tayari kukabidhi ofisi za klabu hiyo na kuiachia nafasi aliyokuwa akikaimu.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Mwalusako alisema ataondoka katika klabu hiyo iwapo uongozi wa klabu hiyo utamtaka kufanya hivyo mara baada ya ujio wa Katibu Mkuu mpya wa klabu hiyo Patrick Naggi.
Alisema kwa sasa bado anaendelea kufanya kazi na kushikilia wadhifa alionao kwa kuwa hakuna kiongozi yeyote aliyeongea naye kuhusu ujio wa katibu mpya.
Alisema licha ya katibu huyo kwenda makao makuu ya klabu hiyo kujitambulisha kuwa ameajiriwa kama Katibu Mkuu hakuna kiongozi yoyote aliyeongea naye wala kumpa maelezo ya aina yoyote.Alisema yeye bado yupo ofisini na hajatambulishwa mtu yoyote hadi jana ,ila kama watakuja na kumleta na kumtambulisha yeye atakabidhi ofisi na kuendelea na shughuli zake nyingine.
Kwa upande wa wanachama wa klabu hiyo, walisema hawatambui ujio wa katibu huyo na hakuna kiongozi yoyote mwenye mamlaka ya kuajiri bila kuwashirikisha wanachama.Wakizungumza katika makao makuu ya klabu hiyo jana, wanachama hao walisema ujio wa Katibu huyo ni mwanzo wa kuvurugika kwa klabu hiyo ikiwa ni pamoja na kuendeshwa kwa kufuata mwongozo wa mtu mmoja.
Kauli ya Mwalusako na wanachama hao imekuja siku moja baada ya Baraza la Wazee la klabu hiyo kutoa tamko la kumpinga katibu huyo kufanya kazi za klabu hiyo.Katibu wa Baraza la Wazee la klabu hiyo, Ibrahim Akilimali, alisema wanamtambua Mwalusako kuwa ndiye mtendaji wa klabu hiyo na si Naggi.
Akilimali alisema kwa mujibu wa katiba ya Yanga endapo kunahitajika mabadiliko ya kiutendaji kunaitishwa kikao cha Kamati ya Utendaji kujadili suala hilo, jambo ambalo halikufanyika.
Naggi aliripoti juzi katika klabu hiyo na kujitambulisha kuwa Katibu Mkuu mpya wa klabu hiyo kwa kuchukua nafasi ya Mwalusako aliyekuwa akikaimu, ambapo katibu huyo aligonga mwamba baada ya wanachama kukataa na kudai kutomtambua.

No comments:

Post a Comment