19 September 2013

KINANA AMPA RUNGU MPINA KUWABANA MAWAZIRI



 Na Mwandishi Wetu, Simiyu
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, amewataka wabunge wa chama hicho kuwahimiza mawaziri ili waweze kutimiza wajibu wao wa kutumikia wananchi tofauti na ilivyo sasa ambapo wengi wao wanafanya kazi kwa mazoea
. Kinana alisema kasi ya kufuatilia utendaji kazi wa mawaziri inayofanywa na Mbunge wa Kisesa (CCM), Luhaga Mpina ni ya kuridhisha na kwamba chama hicho kinaheshimu msimamo wa mbunge huyo katika kuisimamia kikamilifu Serikali ili iweze kutimiza malengo ya kuwaletea maisha bora Watanzania.
Alisema Mpina ni mbunge hodari na jasiri aliyemstari wa mbele kuwatetea wananchi na kuhoji uwajibikaji wa Serikali awapo bungeni, hivyo chama hicho kitaendelea kuthamini mchango wake kwani kwa kiasi kikubwa unasaidia kuharakisha utendaji wa Serikali.
"Mbunge wenu ni hodari, sisi chama tunamheshimu, ni mchapakazi, mtetezi wenu na tunaamini mtaendelea kumchagua katika Uchaguzi Mkuu ujao,"alisema Kinana. Alisema matatizo mengi ya wananchi yanashindwa kutatuliwa kutokana na Mawaziri kukaa maofisini bila kufika katika maeneo husika na kwamba ufuatiliaji wa Mbunge huyo kwa kiasi kikubwa utasaidia kuwaamsha ili waweze kuchapa kazi inayotegemewa na wananchi.
Pia alisifu uwajibikaji wa Mkuu wa Wilaya ya Meatu, Rosemary Kirigini katika kufuatilia kero za wananchi na kuwataka viongozi wengine kuacha kusubiri hadi madhara yatokee ndipo wakimbilie kwenye maeneo hayo kutafuta suluhu.
Kwa upande wake Mpina alisema mapokezi makubwa aliyopata Katibu Mkuu huyo wa CCM ni ishara tosha kuwa Serikali imekuwa ikiwajibika kwa wananchi hasa katika jimbo hilo kwa kufanikisha kutelekezwa kwa ahadi za Rais Jakaya Kikwete alizotoa kwenye kampeni ikiwa ni pamoja na ujenzi wa daraja la Mongo-obakima ambapo wananchi walipoteza maisha kwa kuliwa na mamba na viboko pamoja na kusombwa na maji.
Katika mkutano huo wananchi hao walimuomba Katibu Mkuu huyo wa CCM kuwatafutia suluhu ya tatizo la malisho ya mifugo hususan kwa wananchi wanaoishi kando ya pori la akiba la Maswa kutokana na baadhi ya viongozi kuwabambikia kesi na kuwakamua fedha zao kupitia mgogoro huo wa malisho ya mifugo.
Kufuatia ombi hilo Kinana aliwaagiza Mawaziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki na Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka kufika katika eneo hilo na kuutafutia ufumbuzi mgogoro huo.

No comments:

Post a Comment