09 September 2013

POULSEN AELEZA SABABU ZA KUFUNGWA



Na Mwandishi Wetu, Gambia
KOCHA Mkuu wa timu ya taifa (Taifa Stars), Kim Poulsen amesema kukosekana kwa wachezaji tisa muhimu ni mojawapo ya sababu za kushindwa mechi ya Jumamosi na akaiomba TFF kuhakikisha kuwa wachezaji wanaocheza nje wakiitwa wanakuja nyumbani kucheza.

Poulsen aliyasema hayo mjini Banjul nchini hapa, mara baada ya mchezo na Gambia ambapo wenyeji walishinda kwa mabao 2-0 katika mechi ya mwisho ya kuwania kucheza fainali za Kombe la Dunia.Alisema alikosa wachezaji tisa muhimu, ambapo wengine hawakufika kabisa kutoka wanakocheza soka la kulipwa na wengine walikuwa majeruhi."Nimeambiwa Gambia waliita wachezaji 11 kutoka nje kwa sababu walitambua umuhimu wa kushinda mechi hii na sisi tulikosa karibu timu nzima," alisema.
Alisema ni bora TFF wahakikishe wachezaji hao wanapohitajika hasa kwenye mechi za kufuzu kucheza Kombe la Afrika, wanapatikana kwa wakati."Tumeijenga hii timu tukiwa na malengo ya kufuzu kucheza fainali hizo za Kombe la Afrika kwa hivyo ni muhimu mno wawepo wanapoitwa," alisema Poulsen.
Wachezaji wazoefu wa Stars waliokosa mechi hiyo ni, Mbwana Samatta, Thomas Ulimwengu, Kelvin Yondani, Athuman Idd, Salum Abubakar, John Boko, Mwinyi Kazimoto, Shomari Kapombe na Aggrey Morris.Alisema baadhi yao ambao ni vijana, wamejipatia uzoefu mkubwa pamoja na kwamba walifanya makosa kadhaa uwanjani, ambayo anaamini kama wachezaji wenye uzoefu wangekuwepo wangeweza kudhibiti ile hali kwa namna moja au nyingine.
Hata hivyo, alisema licha ya timu yake kushindwa na Gambia, hajakata tamaa kwani malengo aliyojiwekea tangu mwanzo ni kufuzu kucheza fainali za Kombe la Afrika 2015, jambo ambalo hata TFF na mdhamini,Kilimanjaro Premium Lager wanalitambua na wanaunga mkono.
Kocha huyo alisema inasikitisha kupoteza mechi, lakini Watanzania lazima waelewe kuwa malengo ni ya muda mrefu na timu inaendelea kuimarika siku hadi siku.Alisema huu si muda wa kulaumu na kukata tamaa, kwani safari bado ndefu na tayari kuna dalili nzuri zinaonekana hasa tangu, Taifa Stars ipate udhamini mpya wa Kilimanjaro Premium Lager, ambao unawezesha mambo mengi kufanyika sasa kwani imewekeza zaidi ya sh. bilioni 15 kwa miaka mitano.
"Mechi hizi za Kombe la Dunia zimetupa uzoefu kwani tumeweza kucheza na timu kubwa kama Ivory Coast na Morocco na kuonesha uwezo mkubwa zaidi na hii inaonesha kuwa timu imeimarika kabisa," alisema.Kabla ya mechi hiyo, baadhi wa wananchi wa Gambia walionesha kutokuwa na imani na timu yao baada ya kutofanya vizuri katika mechi zilizopita.
Geoffrey Kaishozi ambaye ni Mtanzania anayefanya kazi Gambia, alisema alifurahishwa na jinsi Stars ilivyocheza katika kipindi cha kwanza, lakini cha pili mchezo ulibadilika baada ya Gambia kupata bao dakika ya 45 na lingine katika kipndi cha pili."Tumesikitika kuwakosa wachezaji wengi tuliowazoea na pengine kuwepo kwao kungeleta utofauti katika mechi hii," alisema na kuongeza kuwa ni vema wachezaji wale muhimu wawepo katika mechi kama hizi.
Naye Francis Mushi alisema alikwenda uwanjani na matumaini kuwa Taifa Stars, ingeshinda hasa baada ya kuifunga Gambia mabao 2-1 katika mechi ya awali nyumbani."Tulicheza vizuri kipindi cha kwanza, lakini cha pili tulilemewa na tukaamka dakika za mwisho za mpira; lakini hatukufanikiwa kupata bao," alisema.
Alisema Gambia pia hawakucheza katika kiwango chao cha kawaida kwa hivyo wengi walitegemea Taifa Stars ingeshinda.Kwa upande wake, Emmanuel Mtaki ambaye pia anafanya kazi Gambia, alisema kulikuwa na makosa mbalimbali kama mabeki kutowadhibiti vizuri wapinzani wao.
Mabao yote ya Gambia katika mchezo huo wa Jumamosi, yalifungwa na nahodha wa timu hiyo, Mustafa Jarjue ambaye alicheza mpira wa hali ya juu.Stars inatarajiwa kuwasili nchini leo saa 8 mchana kwa ndege ya Shirika la Ndege la Kenya.

No comments:

Post a Comment