24 September 2013

HOFU YA MLIPUKO ZANZIBAR



   Siku chache baada ya Padri Anselm Mwang’amba wa Kanisa Katoliki, Parokia ya Machui, Zanzibar kumwagiwa tindikali na watu wasiofahamika, hofu nyingine imeibuka visiwani humo, anaripoti Mwajuma Juma, Zanzibar.

    Hofu hiyo inatokana na mlipuko wa bomu la kienyeji ambao umetokea saa 8:45 usiku wa kuamkia jana katika eneo la Darajani, Wilaya ya Mjini Unguja.
   Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Mkadam Khamis Mkadam, alisema bomu hilo ambalo limetengenezwa kienyeji, lililipuka jirani na duka la Sahara Store.
   “Bomu hili lilirushwa na watu wasiofahamika waliokuwa katika gari aina ya Pick Up ambayo namba zake hazikuweza kupatikana kirahisi, yenye rangi ya silver (fedha)...watu hao walirusha kitu mfano wa soseji na kuangukia kreti za chupa za soda,” alisema.
   Aliongeza kuwa, kwa mujibu wa mlinzi mmoja aliyekuwepo eneo hilo, Bw. Amour Kassim Amour, alisema kitu hicho baaada ya kurushwa, kilianza kutoa moshi mwingi, mshindo mkubwa na kuchimba eneo kilipoangukia bila kuleta madhara.
  “Hakuna mtu aliyekufa wala kuumia, tunaomba wananchi wawe watulivu, waendelee na shughuli zao kama kawaida, Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama tumeinarisha ulinzi katika maeneo yote,” alisema.
Aliongeza kuwa, hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa kuhusishwa na tukio hilo, upelelezi unaendelea.Kamanda Mkadam aliwataka wananchi watoe ushirikiano kwa jeshi hilo na kutoa taarifa zitakazosaidia kuwakamata wahusika ambao lengo lao ni kuleta hofu na taharuki.

No comments:

Post a Comment