24 September 2013

12 WAFA AJALINI MBEYA, DODOMA



 Watu 12 wamefariki dunia katika ajali mbili tofauti ambazo zimetokea mikoa ya Mbeya, Dodoma usiku wa kuamkia jana.
Katika ajali ya kwanza, watu sita wamefariki dunia mkoani Mbeya na wengine saba kujeruhiwa vibaya baada ya gari walilopanda aina ya Toyota Hiace yenye namba T 223 AGQ kuacha njia, kupinduka na kutumbukia mtoni, anaripoti Esther Macha, Mbeya na Elizabeth Joseph, Dodoma.

Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi mkoani humo, Kamishna Msaidizi wa Polisi, Diwani Athuman, alisema ajali hiyo imetokea Septemba 22 mwaka huu, saa mbili usiku, Barabara ya Sokomatola/Stendi Kuu, jijini humo.
Alisema gari hilo lilikuwa likiendeshwa na dereva aliyemtaka kwa jina la Dunia Francis (38), mkazi wa Air Port, jijini humo ambaye ni miongoni mwa majeruhi.
“Waliofariki ni wanawake wawili na wanaume wanne ambao wote hawajafahamika majina yao wala anuani zao...majeruhi ni Juma Warioba (32) mkazi wa Sae na Mwandela Mwamsi (22), mkazi wa Majengo.
“Wengine ni Kambi Ally (32), mkazi wa Iringa, Seleman Shelukindo (25), mkazi wa Ileje, Nuru Shelukindo (32), mkazi wa Ileje na Bahati Ally (14) mkazi wa Songea ambapo wote wamelazwa Hospitali ya Rufaa hapa Mbeya,” alisema.
Kamanda Athumani alisema, breki za gari hilo zilikataa hivyo kupoteza mwelekeo, kupinduka na kutumbukia katika mto uliopo jirani na Stendi Kuu.
“Bado tunaendelea kuchunguza chanzo cha ajali, miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa Mbeya kwa ajili ya utambuzi, dereva anahojiwa,” alisema.
Wakati huo huo, watu sita wamefariki dunia papo hapo na wengine 17 kujeruhiwa baada Basi la Kampuni ya Alsaedy, lenye namba T 433 BLR, walilokuwa wamepanda, kugongana na lori namba T 1O2 CGR, eneo la Chinagali 2 Wilaya ya Chamwino, mkoani Dodoma.
Akizungumzia ajali hiyo, Mratibu Mwandamizi wa Polisi, Damas Nyanda, alisema ilitokea Septemba 22 mwezi huu, saa 3:30 usiku, Barabara Kuu ya Dodoma- Morogoro.
Basi hilo lilikuwa likitokea Dar es Salaam kwenda Dodoma na lori lilikuwa likitoka Dodoma kwenda Dar es Salaam.
Waliokufa katika ajali hiyo ni Nizar Khan (45 ), ambaye ni dereva wa basi, mkazi wa Dar es Salaam, Hassan Kizigo (30-35), ambaye ni dereva wa lori, mkazi wa Temeke, Dar es Salaam.
Wengine ni Ahmad Mohamed (35-40), ambaye ni mmiliki wa lori, mkazi wa Kinyerezi, Dar es Salaam, Hussein Mashauri(35-40) mkazi wa Kinyerezi, Imran Sharif (20-25) ambaye ni utingo wa lori, mkazi wa Jijini Dar es Salaam na abiria mmoja wa basi mwanaume (30-35) ambaye jina lake halijafahamika.
Aliongeza kuwa, chanzo cha ajali ni mwendo kasi wa dereva wa basi ambaye alishindwa kulimudu na kusababisha magari hayo kugongana uso kwa uso.
“Kati ya majeruhi 17, wanaume 10 na wanawake saba, wote wamelazwa katika Hospitali ya Rufaa Dodoma, miili ya marehemu imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti hospitalini hapo ikisubiri utambuzi zaidi,” alisema

No comments:

Post a Comment