28 August 2013

WAZIRI MAHANGA AWASHUKIA WAAJIRI SEKTA BINAFSI



 Na Mwandishi Wetu, Njombe
NAIBU Waziri wa Kazi na Ajira, Dkt. Makongoro Mahanga, amesema Serikali haitaivumilia sekta binafsi yoyote ambayo itawalipa wafanyakazi wake kiwango cha mishahara pungufu ya kile cha kima cha chini kilichotangazwa na Serikali.

Dkt. Mahanga alitoa kauli hiyo kwa nyakati tofauti hivi karibuni alipokutana na wafanyakazi na viongozi wa Kiwanda cha Maziwa cha CEFA kilichopo Njombe pamoja na wale wa mashamba ya Chai Lupombe.
Alisema kiwango cha chini kilichotangazwa na serikali ni kiwango elekezi kinachopaswa kufuatwa na sekta zote na kwamba waajiri wanaweza kulipa zaidi ya viwango hivyo.
Aliongeza kuwa, wizara yake imekuwa ikipokea malalamiko k u t o k a kwa b a a d h i y a wafanyakazi kupitia vyama vyao kwa upande mmoja; na waajiri kwa upande mwingine, kuhusu viwango vilivyotangazwa na serikali kupitia Waziri wa Kazi na Ajira kwenye baadhi ya sekta.
Alifafanua kwamba viwango hivyo vilitangazwa na Waziri baada ya kupata ushauri kutoka kwa Baraza la Ushauri la Kazi na Huduma za Kiuchumi na Kijamii (LESCO) ambalo nalo lilipitia taarifa ya utafiti na mapendekezo ya kitaalamu.
Dkt. Mahanga alisema badala ya vyama hivyo kukimbilia kwa Waziri, wangekaa na waajiri wa kampuni mmoja mmoja na kujadili tija na uzalishaji kwenye makampuni hayo.
"Kama kitaalamu itaonekana viwanda hivyo vina uwezo wa kulipa viwango zaidi ya vile vilivyotangazwa, basi waajiri na wafanyakazi wakubaliane, kupitia Mikataba ya Hiari (CBA), kulipa mishahara hiyo ya juu; na Serikali itatambua mikataba na makubaliano kama hayo," alisema Dkt. Mahanga.
Mwezi wa sita mwaka huu, Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka, alitangaza viwango vya kima cha chini cha mishahara kwenye sekta mbalimbali. Katika tangazo hilo kima cha chini kinaanzia sh. 80,000 kwa mwezi kwa wafanyakazi wa majumbani, sh. 100,000 kwa sekta za kilimo, viwanda na ulinzi; na kuendelea kwenye sekta mbalimbali hadi sh 400,000 kwa mwezi kwa sekta za nishati, utafiti na uchimbaji wa madini na sekta ya fedha.
Hata hivyo, kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wafanyakazi kwa baadhi ya sekta kama viwanda wakidai viwango walivyopangiwa vya sh 100,000 ni vya chini mno.

No comments:

Post a Comment