28 August 2013

VYAMA VYAMTAKA JAJI MUTUNGI KUCHAPA KAZI



 Penina Malundo na Leah Daudi
BAADHI ya viongozi wa vyama vya siasa wamemtaka msajili mpya wa vyama vya siasa nchini, jaji Francis Mutungi atekeleze majukumu yake bila upendeleo kwa chama chochote.Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu jana, Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) Tanzania Bara, Julius Mtatiro alisema kuwa msajili mpya anatakiwa kufanya kazi yake kwa umakini bila kupendelea chama kimoja.

Mtatiro alisema, Msajili huyo akionesha hali ya upendeleo kwa chama kimoja hawatasita kumweleza ukweli.Alisema kuwa, Msajili aliyepita (John Tendwa) alionesha wazi kupendelea chama kimoja ambapo vyama vingine viliondoa uaminifu katika ufanyaji kazi wake.
“Msajili huyu ni mpya, anatakiwa atekeleze majukumu yake vizuri na kutoonesha hali yoyote ya upendeleo, kwa baadhi ya vyama na endapo ataonesha hali hiyo hatutaogopa kumueleza waziwazi kwa kitendo atakachokifanya,” alisema Mtatiro.
Naye Katibu Mkuu wa Chama cha NCCR Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema kuwa msajili mpya anatakiwa kusimamia vyama vya siasa kwa ukaribu na kujua changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika vyama.
Pia alisema, changamoto hizo anapaswa kuzitatua ili kuweza kuleta hali ya upendo na amani katika vyama vya siasa.“Tumefurahi kupata msajili mpya wa vyama vya siasa nchini, hivyo tunamuomba afanye kazi kwa ufasaha na kwa umakini zaidi, ili kuweza kuondoa changamoto zilizopo katika mambo ya usajili wa vyama,” alisema Nyambabe.
Aidha, aliongeza kuwa Msajili mpya anapaswa kuboresha kanuni mbalimbali za usajili wa vyama, kwani asilimia kubwa ya kanuni hizo zimepitwa na wakati na kanuni nyingine hazioneshi wazi kuwa zinahitaji nini.

No comments:

Post a Comment