27 August 2013

WATAKA RASIMU IFAFANULIWE KIKAMILIFU



 Na Lilian Justice, Morogoro
WAKAZI wa kata tatu za Manispaa ya Morogoro wameiomba Serikali kupitia baraza la katiba kuhakikisha marekebisho ya rasimu ya Katiba Mpya yanafafanua kwa kina masuala ya kijamii ikiwemo kipengele cha afya, elimu na maji kufuatia vipengele vingi kukosa ufafanuzi.

Wakazi hao walisema hayo mwishoni mwa wiki kwenye tamasha la sanaa ya uhamasishaji wananchi juu ya uchangiaji maboresho ya rasimu ya Katiba Mpya lililoandaliwa na Shirika lisilo la kiserikali la Mapinduzi Forum kwa kushirikiana na Shirika la Mkitunda baada ya kupewa baraka na Tume ya baraza la katiba kupitia ufadhili wa The Foundation For Civil Society na kufanyika katika kata tatu za Manispaa ya Morogoro ambazo ni Kihonda, Mazimbu na Mafisa.
Maimuna Mabeja ni mmoja kati ya wananchi waliopata nafasi ya kushiriki matamasha hayo na kutoa maoni yao ambapo aliomba baraza la katiba kuhakikisha linatoa kipaumbele katika masuala ya jamii ikiwemo afya, elimu na maji kwa kutoa ufafanuzi wa kina ili kuifanya jamii kujua umuhimu wao katika masuala hayo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa shirika la mapinduzi Forum ambaye pia ni Msimamizi wa mradi huo, Mkosasura Waziri alisema kuwa katika kuhakikisha wananchi wanapata nafasi ya kuchangia maboresho ya rasimu ya Katiba Mpya Mapinduzi imeamua kufanya sanaa shirikishi katika kata hizo kwa kufanya maigizo, ngoma na kuibua mada ambazo wananchi wameweza kuchangia ili kuboresha rasimu ya Katiba Mpya.
Waziri alisema kuwa mpaka sasa tayari wameshagawa rasimu za katiba 140 kwa wananchi wa kata hizo ambao wameshazipitia na kutoa maoni yao ambapo wanatarajia kugawa rasimu za katiba 130 kwa wananchi watakaochaguliwa kushiriki katika mdahalo waliouandaa utakaofanyika Agosti 26 na 27 mwaka huu ili wananchi waweze kutoa maoni yao katika maboresho hayo.
Hata hivyo kwa upande wa Ofisa Tawala wa shirika hilo, Zainabu Mkali alisema kuwa uhamasishaji huo utasaidia wananchi hasa wale waliokosa nafasi ya kuchangia maoni ya katiba mpya kuweza kutoa maoni yao katika maboresho ya rasimu ya katiba mpya kupitia sanaa wanayoitoa.

No comments:

Post a Comment