Na Pamela Mollel,
Arusha
JESHI la Zimamoto na Uokozi Mkoa wa
Arusha limeanzisha utaratibu wa kutoa mafunzo ya namna ya kuzima moto na uokozi
katika shule za msingi na sekondari.Lengo la
mafunzo hayo ni kujikinga na kukabiliana na majanga mbalimbali yanayotokana na
moto na uokozi ikiwa ni hatua ya kuelimisha makundi mbalimbali ya kijamii
kuchukua hatua za mapema kuepuka madhara makubwa.
Hayo yameelezwa
juzi na Mkuu wa kikosi hicho mkoani hapa, Kamishna Msaidizi, Jesuald Ikonko
alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kabla ya kuanza
uzinduzi wa zoezi la kutoa mafunzo hayo ya kuzima moto na uokozi kwa wanafunzi
wote jijini hapa.
Alisema kuwa, jeshi
hilo linatoa mafunzo katika shule mbalimbali za msingi na sekondari kwa lengo
la kuwajengea uelewa wanafunzi na walimu kwa kuwapatia mbinu sahihi ya kuchukua
hatua za mapema pindi linapotokea janga la moto na maafa mengine katika shule.
Ikonko alisema
kutokana na jamii kutokuwa na elimu ya kutosha moto huo unapotokea katika shule
au taasisi zingine na sehemu za makazi umekuwa ukisababisha madhara na majanga
makubwa ikiwemo kuteketeza mali na vifaa mbalimbali kunakotokana na ukosefu wa
mbinu za kukabiliana na moto huo.
Alisema kuwa, kutokana
na kuongezeka kwa matukio ya moto na kuteketeza maeneo mbalimbali Jeshi la
Zimamoto na Uokozi, limeanzisha kitengo maalumu cha kutoa elimu ya kukabiliana
na majanga ya moto katika maeneo mbalimbali ya makazi, zikiwemo taasisi na
shughuli zingine za kiuchumi.
Mafunzo hayo
yanatolewa kwa awamu tofauti tofauti, ambapo awamu ya kwanza ya mafunzo hayo
ambayo ni mwendelezo wa mafunzo kama hayo itahusisha shule nne za Uhuru,
Edmundrise, St. Thomas na Ilboru sekondari zote za jijini Arusha na awamu
zingine zitahusisha shule, taasisi mbalimbali na wananchi mkoani Arusha.
"Elimu hiyo
kupitia kwa wanafunzi itawafikia wananchi wengi, hivyo kuepuka majanga
yanayotokana na moto. Pia wananchi wanaweza kutoa taarifa popote pale ukitokea
moto wapige namba 114 au 0252333 bure bila malipo," alisema.
Alisema, watoto wamekuwa wakichezea viberiti, mishumaa na vitu ambavyo
ni visababishi vinavyoweza kupelekea hatari ya moto kutokea hivyo elimu hiyo
itawasaidia kuwa makini na kuchukua tahadhari
No comments:
Post a Comment