02 August 2013

WANAFUNZI KUFUNDISHWA MBINU ZA KUJIKINGA MOTO



 Na Pamela Mollel, Arusha
JESHI la Zimamoto na Uokozi Mkoa wa Arusha limeanzisha utaratibu wa kutoa mafunzo ya namna ya kuzima moto na uokozi katika shule za msingi na sekondari.Lengo la mafunzo hayo ni kujikinga na kukabiliana na majanga mbalimbali yanayotokana na moto na uokozi ikiwa ni hatua ya kuelimisha makundi mbalimbali ya kijamii kuchukua hatua za mapema kuepuka madhara makubwa.

Hayo yameelezwa juzi na Mkuu wa kikosi hicho mkoani hapa, Kamishna Msaidizi, Jesuald Ikonko alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kabla ya kuanza uzinduzi wa zoezi la kutoa mafunzo hayo ya kuzima moto na uokozi kwa wanafunzi wote jijini hapa.
Alisema kuwa, jeshi hilo linatoa mafunzo katika shule mbalimbali za msingi na sekondari kwa lengo la kuwajengea uelewa wanafunzi na walimu kwa kuwapatia mbinu sahihi ya kuchukua hatua za mapema pindi linapotokea janga la moto na maafa mengine katika shule.
Ikonko alisema kutokana na jamii kutokuwa na elimu ya kutosha moto huo unapotokea katika shule au taasisi zingine na sehemu za makazi umekuwa ukisababisha madhara na majanga makubwa ikiwemo kuteketeza mali na vifaa mbalimbali kunakotokana na ukosefu wa mbinu za kukabiliana na moto huo.
Alisema kuwa, kutokana na kuongezeka kwa matukio ya moto na kuteketeza maeneo mbalimbali Jeshi la Zimamoto na Uokozi, limeanzisha kitengo maalumu cha kutoa elimu ya kukabiliana na majanga ya moto katika maeneo mbalimbali ya makazi, zikiwemo taasisi na shughuli zingine za kiuchumi.
Mafunzo hayo yanatolewa kwa awamu tofauti tofauti, ambapo awamu ya kwanza ya mafunzo hayo ambayo ni mwendelezo wa mafunzo kama hayo itahusisha shule nne za Uhuru, Edmundrise, St. Thomas na Ilboru sekondari zote za jijini Arusha na awamu zingine zitahusisha shule, taasisi mbalimbali na wananchi mkoani Arusha.
"Elimu hiyo kupitia kwa wanafunzi itawafikia wananchi wengi, hivyo kuepuka majanga yanayotokana na moto. Pia wananchi wanaweza kutoa taarifa popote pale ukitokea moto wapige namba 114 au 0252333 bure bila malipo," alisema.
Alisema, watoto wamekuwa wakichezea viberiti, mishumaa na vitu ambavyo ni visababishi vinavyoweza kupelekea hatari ya moto kutokea hivyo elimu hiyo itawasaidia kuwa makini na kuchukua tahadhari  

No comments:

Post a Comment