Reuben Kagaruki
MIMI kutolala na mke wangu kunatokana na
yeye kuninyima tendo la ndoa..., kila ninapolala kwake nakuwa kama
niko kwenye lindo, hanipi unyumba kabisa, kamwe sikubali. Kama
mwenzangu ana mahali anakomalizia shida yake, basi aseme
.Kauli hiyo ni ya mkazi wa Kata ya Nachingwe wilayani
Ruangwa, Mohamed Said Ndende, ambayo aliitoa mbele ya Mtendaji wa Kata ya
Nachingwe wilayani Ruangwa Rajab Macholilo, akizungumzia mgogoro wake na mkewe.
Ndende anasema amekuwa akimsaidia kulima isipokuwa
anachodai, Darlin Hassan (mke wake) maarufu kwa jina la Bibi Dogo labda ni
suala la ngono tu yaani kutotimiziwa tendo la ndoa.
Ndende, anakiri kwamba Bibi Dodo ni mkewe na wameishi naye
kwa miaka mingi. Akitoa ushuhuda wa tukio la kutelekezwe na mume wake, Bibi
Dogo anasema;
“Nimezaa na mume wangu huyo (Ndende) watoto watano na sasa
hivi ni wakubwa. Tumeishi naye kwa zaidi ya miaka 40. Wazee wametukalisha vikao
kadha wa kadha wakimsihi anihudumie mimi na watoto wetu hao, lakini hafanyi
hivyo, tabia yake haibadiliki.
L a k i n i s i w e z i kumfunga ninachohitaji ni haki yangu
tu,” anasema Darlin kwa masikitiko.
Anaongeza kuwa: “Aliwaambia ndugu zangu eti amepata mke mwingine.
Mpaka sasa tuko wake watatu, mke wake wa pili alifariki na sasa anaishi na mke
wake wa tatu.
Nimemwambia tukakae wote huko, lakini hataki...namtaka
anitimizie mahitaji yangu ya ndani na anisaidie kulima, lakini hataki,” alizidi
kulalamika.
Kilio cha mwanamke huyo ni kielelezo cha matatizo
yanayotokea ndani ya ndoa hadi kufikia hatua ya wanawake kutelekezwa na
kujikuta wakibaki na jukumu la kutunza familia.
Hali hiyo inatokea hapa nchini ikieleweka wazi kuwa wanaume
ndiyo nguzo ndani ya familia yoyote. Mara nyingi nguzo hiyo muhimu ndani ya
familia inaposhindwa kutimiza wajibu wake familia inayumba na kupoteza
mwelekeo.
Leo hii watoto wengi wanaishi katika mazingira magumu
kutokana na wanaume kushindwa kutimiza wajibu wao. Tatizo hili ingawa linachangiwa
na vifo, lakini kwa upande mwingine linachangiwa na wanaume kutelekeza familia
zao.
Mfano, kati ya kesi zinazoongoza kwenye mabaraza ya
usuluhishi kwenye kata ni zile za wanaume kutelekeza familia. Mara nyingi
inapotokea migogoro kwenye familia waathirika wakubwa ni wanawake na watoto.
Utafiti uliofanywa na Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania
(TAMWA) kwa kushirikiana na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Chama cha
Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA), Chama cha Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA)
na Kituo cha Usuluhishi cha TAMWA (CRC) kwenye mpango wa kutokomeza ukatili na
unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto (GEWE II) katika wilaya 10
za Tanzania bara na Zanzibar umeweza kubaini ukubwa wa tatizo la wanaume
kutelekeza wanawake na watoto.
Wilaya za Utafiti zilikuwa ni Wete, Unguja Mjini Magharibi
na Unguja Kusini.
Zingine ni Kinondoni na Ilala Kisarawe, Mvomero, Ruangwa na
Lindi Vijijini na Newala.
Utafiti umeonesha wazi kuwa moja ya matukio ambayo
yanayoonekana kushamiri katika jamii ni wanaume kutelekeza wanawake zao na
watoto.
Kwa
mujibu wa utafiti, sababu zinazowafanya wanaume watelekeze wake wao ni kukosa
uaminifu, ugomvi usioisha na maisha magumu hasa pale wilaya ama eneo husika
linapokumbwa na baa la njaa.
Utafiti
umebaini kuwa tatizo hili lipo katika wilaya zilizofanyiwa utafiti yaani tatu
za Zanzibar na
saba za Tanzania Bara.
Baadhi
ya sababu zinazochangia ni kutotumika ipasavyo kwa sheria zinazaowalinda
wanawake na watoto kama sheria ya mtoto ya
mwaka 2009, jamii kutokuwa na elimu ya ndoa hivyo wanaume kuutumia vibaya
uongozi ndani ya familia zao, vipigo ndani ya ndoa, rushwa kutawala katika
vyombo husika, kukosekana uaminifu ndani ya ndoa talaka na kupotea kwa maadili
katika jamii.
Athari
za wanawake na watoto kutekelezwa, ni watoto kukosa malezi ya wazazi wawili,
kuacha masomo kutokana na ugumu wa maisha na kulazimika kuingia kwenye ajira
mbaya ikiwemo uasherati na kazi ngumu kama
vile kupasua kokoto ili kuingiza kipato katika familia zao.
Aidha,
wanawake kubebeshwa mzigo mkubwa wa kutunza familia na kuwafanya kurudi nyuma
kimaendeleo, kuongezeka umaskini, familia kusambaratika na wanawake kukosa haki
zao.
Katika
wilaya tatu za Zanzibar, jumla ya matukio ya
utelekezwaji wanawake ni kama ifuatavyo;
Katika Wilaya ya Wete kulikuwa na 131, Magharibi 239, Kusini Unguja 11. Chanzo
cha takwimu hizo ni Dawati la Jinsia.
Hata
hivyo, imeelezwa kuwa baadhi ya waathirika hawaripoti matukio ya udhalilishaji
katika mamlaka husika na hivyo takwimu kuonesha matukio hayo ni machache.
Utafiti
huu pia umebaini kuwa talaka zimechangia kwa kiasi kikubwa wanawake na watoto
kutelekezwa. Jeshi la Polisi Pemba, limethibitisha kuwa tatizo ni kubwa
kutokana na waathirika kutoripoti matukio katika vyombo vya sheria.
Kwa
mfano, jeshi hilo
limesema mwaka 2011, Dawati la Wanawake na Watoto la Polisi Kaskazini Pemba,
lilipokea jumla ya kesi nane ambapo mwaka 2012 kesi sita na kipindi cha Januari
hadi Machi, 2013 ni tukio moja tu lililoripotiwa.
Lak
in i taar if a za wizar a zimebainisha kuwa, Idara ya Ustawi wa Jamii kwa
Wilaya ya Wete, mwaka 2011 ilipokea kesi 12, mwaka 2012 kesi tisa na kati ya
Januari na Machi, 2013, matukio matatu yameripotiwa.
Kwa
upande wa wilaya ya Newala, Katibu wa Mtandao wa asasi zisizokuwa za kiserikali
Wilaya ya Newala mkoani Mtwara, Halima Nambunga, anasema asilimia 60 ya familia
wilayani humo zinalelewa na bibi au mzazi mmoja kutokana na kutelekezwa au
talaka za mara kwa mara.
Mkuu
wa wilaya hiyo, Christopher Magala, anasema utamaduni wa kusafisha ghala au
kuanua umechangia kuongezeka kwa tatizo. “Huu ni utamaduni ambao mwanaume wa
Newala anapopata fedha hasa wakati wa msimu wa korosho, hutoa vitu vyote vya
zamani ndani ya nyumba yake akiwamo mwanamke na kuingiza vitu vipya ikiwamo
kuoa mwanamke mwingine,” alisema Magala.
Magala
anafafanua kuwa utamaduni huo humsababishia mwanamke kutothaminiwa kwa kuwa
utamaduni huo umekuwa ukiwadhalilisha wanawake na kuyumbisha watoto, kwani
wakati huo mtoto atabaki na mama peke yake au kupelekwa kwa bibi yake na hatma
yake watoto kukosa huduma muhimu kutoka kwa wazazi wao.
Hakimu
Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Newala, Samwel Maeda, anasema Sheria ya
Matunzo kwa mtoto imepitwa na wakati kwani hadi sasa faini kwa mwanaume
anayemtelekeza mtoto ni sh. 10,000 jambo ambalo wengi huipuuzia kwani
wanafahamu kwamba watamudu kuilipa.
Kwa
msingi huo, inashauriwa kuwa ipo haja kwa sheria hiyo ifanyiwe marekebisho ili
iendane na wakati pamoja na uzito wa kosa lenyewe.
Watendaji
wa vijiji vyote katika Kata ya Mtibwa Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro,
wanaeleza kuwa wanaume wengi huzitelekeza familia zao wakati wa njaa na kuhamia
vijiji vya mbali, huku wakiwaacha wanawake kuhangaika kuzilisha na kuzitunza
familia peke yao.
Hata
hivyo, wanaume hao hurejea na kuungana na familia zao wakati wa mavuno. Mbaya
zaidi, wanasema baada ya kurejea kwa wanaume hao, huchukua jukumu la kuuza
mazao yaliyolimwa na wanawake na watoto wao na wakishapata fedha, baadhi yao huenda kuoa wanawake
wengine na kuziacha tena familia zao.
Ofisa
Mtendaji wa Kijiji cha Kidudwe, Marco Mwakatundu, anasema amekuwa akipokea
malalamiko ya wanaume kuzikimbia familia zao hasa katika kipindi cha njaa
ambacho mara nyingi ni kati ya Machi na Mei ya kila mwaka.
Ofisa
Mtendaji wa Lukenge wilayani Mvomero, Ally Kingu, anasema kuna umuhimu wa jamii
kuelimishwa juu ya haki na wajibu wao katika familia.
“Wanawake
wanahitaji kuelimishwa juu ya umuhimu wa kujitambua na vile vile wanaume nao
ili wajue haki na wajibu wao katika familia,” anasema.
Hata
hivyo, Mratibu wa Elimu Kata ya Nachingwea (MEK), Benedict Barnabas Nyuchi,
anasema tabia ya baadhi ya wanawake ndiyo chanzo cha wao kutelekezwa kutokana
na kuwajibu waume zao kwa lugha za kijeuri na dharau.
Kwa
mfano, Benedict Barnabas Nyuchi anasema mwanamke anayemjibu mumewe kuwa watoto
wote siyo wake eti kwa kuwa hana uwezo wa kuzaa watoto kama
hao, ni dhahiri atamuudhi mumewe na kusababisha ugomvi.
Katika
mazingira kama haya, ni dhahiri mwanaume hupatwa na hasira na kuamua kuondoka
kumuacha mke na watoto kama si kumpa kipigo
kikali.
No comments:
Post a Comment