02 August 2013

WACHEZAJI WAPYA YANGA HADHARANI



Na Elizabeth Mayemba
KLABU ya Yanga inatarajia kuanika kikosi chake chote keshokutwa watakapocheza mechi yao ya kirafiki na Mtibwa Sugar inayotarajiwa kuchezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.Mechi hiyo imeandaliwa na Chama cha Soka Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA)
.Akizungumza Dar es Salaam jana, Ofisa Habari wa klabu ya Yanga Baraka Kizuguto alisema wachezaji wao wote waliowasajili watakuwa hadharani keshokutwa hata wale ambao walikuwa na timu ya taifa, Taifa Stars nao wamejiunga na wenzao."Ni mechi ambayo tunaitumia kwa ajili ya kuwatambulisha wachezaji wetu wote tuliowasajili, hivyo tunaimani mashabiki wetu watatumia fursa hiyo kuwaona wachezaji wapya," alisema Kizuguto.
Alisema wachezaji wapya ambao hadi sasa wamesajiliwa na klabu hiyo na keshokutwa watacheza ni Mrisho Ngassa, Deogratius Mushi 'Dida', Rajabu Zahir, Hamisi Thabiti, Shaaban Kondo, Ladius Luajo na Hussein Javu.Alisema itakuwa ni nafasi nzuri kwa wachezaji hao kuonesha viwango vyao ambapo wanaamini kabisa mashabiki wao watawafurahia.
Kwa upande wake Mweka Hazina wa DRFA Ally Kobe alisema kwa upande wao wameamua kuandaa mechi hiyo kwa ajili ya kuisaidia timu ya Yanga ambayo ipo chini yao, pia wanaimani na Mtibwa nao itakuwa ni mechi yao nzuri kwa maandalizi ya Ligi Kuu.
"Sisi ni Chama cha Mkoa wa Dar es Salaam na Yanga ipo chini yetu hivyo ni jukumu letu kuwaandalia mechi ya kirafiki ikiwa ni maandalizi ya ligi kuu," alisema Kombe.
Alisema katika mechi hiyo viingilio kwa VIP A ni sh.15,000, VIP B 10,000 na VIP C na viti vingine vilivyosalia kiingilio kitakuwa ni sh.5,000

No comments:

Post a Comment