23 August 2013

TAMBWE AANZA KUTEMA CHECHE SIMBA SC


Na Elizabeth Mayemba

MSHAMBULIAJI mpya wa Simba raia wa Burundi, Hamis Tambwe ameanza kuonesha cheche zake katika klabu hiyo, baada ya juzi kuifungia bao pekee walipocheza na Stand United ya Shinyanga katika mechi ya kirafiki.
Simba walikuwa Kahama na Shinyanga kwa ajili ya kujiandaa na mechi yao dhidi ya Rhino Rangers ya Tabora ya ufunguzi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, itakayochezwa mjini Tabora kesho.Akizungumza kwa simu wakiwa njiani kwenda Tabora, Kaimu Mwenyekiti wa Simba, Joseph Itang'are 'Mzee Kines', alisema waliondoka jana mkoani Shinyanga na walitarajia kufika jioni ya siku hiyo Tabora kwa ajili ya mechi yao ya kesho.

Alisema wakiwa Shinyanga walicheza mechi ya kirafiki na Stand United inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza na kushinda bao 1-0, lililofungwa na Tambwe.Mzee Kines alisema wachezaji wote wapo katika hali nzuri hakuna majeruhi hata mmoja, hivyo inampa wakati mzuri Kocha Mkuu wa timu hiyo, Abdallah 'King' Kibadeni kupanga vizuri kikosi chake.

Akizungumzia uhamisho wa wachezaji wao wa kimataifa, Tambwe na beki Gilbert Kaze Mzee Kines alisema uongozi ulishamalizana na klabu ya Vital'0 na wakati wowote kuanzia sasa vibali hivyo vitatua nchini."Uongozi umeshamalizana na Vital'0 na wakati wowote kuanzia sasa vibali hivyo vitatua nchini na wachezaji hao wataichezea timu yetu, mashabiki wetu na wanachama wasiwe na wasiwasi na hilo," alisema Mzee Kines. Alisema kuna watu wasioitakia mema timu yao na kuzusha maneno mengi kuhusu wachezaji hao wapya, lakini wao hawatishwi na wanapambana na kila changamoto iliyo mbele yao.

No comments:

Post a Comment