06 August 2013

TAKWIMU ZA UFAULU ZISIZUIE SERIKALI KUJENGA SHULE


HIVI karibuni Serikali kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ilitangaza na kutoa takwimu kuhusu wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano katika shule za Serikali na vyuo vya ualimu kwa mwaka huu.Katika taarifa hiyo ya Serikali ambayo ilionesha kuwa kutakuwa na upungufu mkubwa wa wanafunzi 10,074 katika sekondari 207 zinazomilikiwa na Serikali.

Taarifa hizi hazishangazi sana kutokana na matokeo mabovu ya wanafunzi wa kidato cha nne katika mwaka uliopita. Kwani katika matokeo hayo wanafunzi zaidi ya asilimia 60 walifeli mitihani yao na hivyo kuwa gumzo na simanzi kwa serikali, wazazi, wanafunzi, wananchi na Taifa kwa ujumla wake .
Hali katika sekta ya elimu nchini imezidi kuonesha kudidimia kwani kiwango hicho cha kufeli hakikuwahi kutokea katika historia ya nchi yetu.
Kama tujuavyo elimu ni suala mtambuka na linagusa karibu kila sekta nchini ikiwamo sekta ya elimu yenyewe, kilimo na madini. Hivyo kama Serikali itaendelea kufumbia macho elimu ya nchi hii, Taifa halitakuja kupiga hatua ya kimaendeleo katika miaka nenda rudi.
Kutokana na takwimu hizo zilizotolewa na Serikali ambapo imeonesha upungufu mkubwa wa wanafunzi katika shule zinazomilikiwa na Serikali, lakini pia bado athari ya takwimu hizi itaenda mpaka kwenye vyuo vya juu kwa kukosa wanafunzi kwa ajili ya masomo ya ngazi mbalimbali za elimu.
Pamoja n a hayo S e r i k a l i imeshindwa kuongeza shule kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha tano kutokana na sababu hiyo hiyo ya upungufu wa wanafunzi katika shule za Serikali. Kitu kilichonipelekea kuandaa makala haya.
Serikali pia imeshindwa kuongeza shule kwa sababu ambayo ukiiangalia ni ya wazi kabisa ya upungufu uliopo wa wanafunzi lakini nadhani sababu hii si ya msingi sana, kwani upungufu wa wanafunzi kwa mwaka huu haumaanishi itakuwa hivyo mwakani na miaka mingine inayokuja.
Upo msemo hapa unaosema 'bora kuwa nacho kuliko kukosa kabisa', msemo huu una maana kubwa katika hali tuliyonayo. Ni kweli kutokana na matokeo ya kidato cha nne na wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na shule hizo za Serikali zilizopo kuna upungufu mkubwa sana wa wanafunzi katika shule zinazomilikiwa na Serikali.
Lakini hili lisizuie Serikali kujenga shule zingine kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha tano, kwani takwimu hizi zinaweza kubadilika mwakani au katika mwaka wowote ule.
Serikali kupitia kwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi inapaswa kuongeza shule kwa wanafunzi wa kidato cha tano vilevile kwa wanafunzi wa vidato vya chini.
Kujengwa kwa shule hizi kunaweza kusaidia baadaye hasa katika kudahili wanafunzi wachache watakaokidhi katika kila shule kutokana na idadi ya wanafunzi waliofaulu.
Lakini pia hali ya ufaulu inaweza kuongezeka katika mwaka ujao wa masomo au katika miaka mingine na hivyo kukawa na tatizo la wanafunzi kukosa shule hii inawezekana kabisa na kama Serikali itakaa na ikadhani kwamba ufaulu wa wanafunzi utaendelea kushuka basi hali inaweza kuwa mbaya zaidi ya wanafunzi kukosa shule.
Mara nyingi walimu wamekuwa wakilalamika wanafundisha wanafunzi wengi tofauti na namba halisi inayopaswa kuwepo darasani lakini kwa hali ilivyo sasa kwa wanafunzi wa kidato cha tano itabadilika kwani wanafunzi ni wachache ukilinganisha na shule zilizopo.
Wasiwasi wangu ni vipi hali ya mambo itakapobadilika, kwani zipo juhudi za wazazi,walimu na wanafunzi za kutaka kubadilisha hali ya elimu nchini kutokana na matokeo na takwimu hizi mbovu.
Nafikiri ni vyema kwa Serikali kulingana na bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kujenga shule za kutosha za kidato cha tano kwa ajili ya wanafunzi wa miaka inayofuata.
Kama nilivyosema awali ni vyema ukawa nacho kuliko kukosa kabisa, hivyo nazidi kuishauri Serikali kuwa ni bora kuanza mipango ya mapema ya kuongeza shule za kidato cha tano badala ya kungoja ongezeko la ufaulu ndipo waanze na mikakati hii.
Serikali ina jukumu kubwa la kuleta mabadiliko ya sekta ya elimu nchini na likiwemo hili jukumu la kujenga shule za sekondari, vyuo vya ualimu, vyuo vya ufundi na vyuo mbalimbali vya elimu ya juu.
Hivyo basi kulingana na bajeti ya wizara, Serikali ingepaswa kuongeza shule kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha tano, Serikali inapaswa kutekeleza azma hiyo kwani pamoja na matokeo na takwimu zilizotolewa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi bado kuna nafasi ya mabadiliko makubwa katika miaka inayofuata.
Ipo dhana kwamba kutokana na mfumo wetu wa elimu kuna hatari kubwa ya kuendelea kuporomoka kwa viwango vya ufaulu kwa wanafunzi wa kidato cha nne, na kimsingi kabisa nakubaliana nayo, lakini wasiwasi wangu ni vipi hali ikibadilika? Ni vipi katika mwaka huu wanafunzi wa kidato cha nne wakafanya vizuri zaidi katika mitihani yao? Rai yangu kwa Serikali ni kujenga shule zakutosha zenye lengo la kudahili wanafunzi wa kidato cha tano.
Mwandishi wa makala haya ni mwanahabari na mwanafunzi wa Stashahada ya Sheria katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama- Lushoto

No comments:

Post a Comment