06 August 2013

SUMATRA IRINGA YAONGEZA VITUO VIPYA VYA MABASI


OFISA Mfawidhi wa Mamlaka ya Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA) mkoani Iringa, Rahim Kondo amesema mamlaka hiyo katika Manispaa ya Iringa imeongeza vituo vya mabasi.Lengo likiwa ni kuondoa msongamano katika Kituo cha Mabasi Miyomboni ambacho kilionekana kuelemewa kabla ya kufungua stendi nyingine nne na kuwezesha wananchi sasa kupata usafiri kwa urahisi zaidi kuliko hapo awali ambapo walikuwa wanakaa muda mrefu kusubiria daladala zipakie hadi zijae ndipo waondoke.

Akizungumza na Majira ofisini kwake jana, ofisa huyo alisema vituo vya mabasi ambavyo vimeongezwa ni pamoja na Kituo cha Mashine Tatu ambacho kitatumika katika kupakia na kushusha abiria wa daladala za Cgrielo Mashine Tatu, Kiwandani kuja Mashine Tatu na daladala za kwenda Igumbilo kuja Mjini ambapo zitatakiwa kuishia Mashine Tatu.
Alifafanua kuwa, katika kituo cha Mlandege daladala zitapakia na kushusha kutoka Nyabula kuja Iringa Mjini, kituo cha MR Hotel kitatumiwa na daladala za kutoka Mawelewele kuja Mjini, Don Bosco kuja Mjini, kutoka Megic Site kuja Mjini ambapo kituo kipya cha eneo la Posta kitatumika kwa daladala ambazo zinafanya safari ya kutoka Kalenga kuja Mjini na Ipamba kuja Mjini.
Pia amewataka madereva wahakikishe wanazingatia ruti zao bila kuzivuruga.
Akizungumzia sababu ya kuongezwa kwa vituo hivyo, Kondo alisema kuwa abiria walikuwa wanalazimika kusafiri na kulipa nauli zaidi ya mara mbili hadi tatu hali ambayo kwa sasa itawawezesha kutumia nauli moja kufika mjini na hatimaye kuendelea na shughuli zao ambazo wanataka kuzifanya.
"Vituo hivi...kwa kweli vinalenga kupunguza msongamano, kuboresha usafiri kwa abiria, hadi sasa tunafanya uchunguzi wa maeneo mengine ambayo daladala hazifiki tutapima kilomita na tutazisajili daladala zifanye safari zao huko na maeneo yote ya mji wa Iringa tunataka kuhakikisha kunakuwepo usafiri kila wakati ili wananchi watumie muda wao vizuri kufanya shughuli na siyo kukaa kwenye vituo vya mabasi kwa muda mrefu," alisema ofisa huyo wa SUMATRA.
Aliongeza kuwa, suala la kuongeza vituo hivyo vipya limewezesha kupunguza foleni ya kukaa muda mrefu katika kituo kimoja huku daladala zikisubiriana zijaze ambapo kwa sasa kila daladala zitafanya safari kutoka eneo ambalo zimesajiliwa hadi kituo kimoja na kugeuka mara moja.
Hali ambayo itawasaidia abiria huku ikiwaongezea kipato wamiliki wa mabasi na daladala na kutumia muda vizuri.

No comments:

Post a Comment