02 August 2013

SERIKALI YALAUMIWA MRADI WA KIGAMBONI



Na Andrew Ignas
MBUNGE wa Jimbo la Kigamboni, Dkt. Faustine Ndungulile ameiomba Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuzirudisha kata tatu ambazo zilikuwa Manispaa ya Temeke na kuziingiza kweye mradi wa makazi mapya Kigamboni
. Januari mwaka huu, wizara hiyo iliongeza kata tatu ambazo ni Kimbiji, Pemba Mnazi, Kisarawe 2 na sehemu kubwa ya Somangila katika mradi wa ujenzi wa mji mpya wa Kigamboni ambao awali ulianza na kata tano.Kata ambazo zilikuwa ni Kigamboni, Vijibweni, Sehemu ndogo ya Somangila, Kibada, Mji Mwema na Tungi.
Akizungumza na waandishi wa habari juzi, mara baada ya kumalizika kwa Baraza la Madiwani Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Mbunge huyo alisema kuwa serikali ikubali kuzirudisha kata hizo ambazo ziliongezwa katika mpango wa ujenzi huo kwa kuwa hawakuishirikisha manispaa husika.
"Ndugu zangu waandishi iwe...isiwe lazima Wizara izirudishe kata hizo tatu ili kuinusuru halmashauri, sehemu kubwa ya mapato ya Manispaa inatokana na mauzo ya viwanja hivyo hilo lizingatiwe," alisema Dkt. Ndungulile.
Wakati huo huo, Mstahiki Meya wa Manispaa hiyo, Maabadi Suleimani Hoja alisema maombi yao ya kuonana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwa ajili ya kumuomba serikali kuwarudishia Temeke nyongeza ya zile kata tatu zilizoongezwa kwenye mradi huo hayajafanikiwa mpaka sasa licha ya kumuandikia barua.

No comments:

Post a Comment