13 August 2013

SERIKALI IPUNGUZE KODI SERENGETI



 Na Anneth Kagenda
SERIKALI imetakiwa kuacha kutoza kodi kubwa kwenye milango ya kuingia na kutoka katika Hifadhi ya Taifa Serengeti iliyopo wilayani Serengeti Mkoa wa Mara kwa madai kufanya hivyo ni kuwaumiza wananchi wa kipato cha chini.

Wito huo ulitolewa Dar es Salaam jana na Mbunge wa Jimbo la Serengeti, Dkt. Stephen Kebwe wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii katika Ukumbi Mdogo wa Bunge kwenye Kamati za Bunge zilizoanza jana jijini hapa.
Alisema, ni muda mwafaka kwa serikali kuliangalia upya jambo hilo kwani si vema wananchi kuendelea kukamuliwa kwa kodi kubwa badala yake wawaachie hizo hizo zilizokuwepo na kuhoji wafanyabiashara kutolipa kodi badala yake wanapita kwenye milango hiyo kiujanja.
"Awali kodi ya kupita getini kwa mwananchi mmoja ilikuwa sh. 1,500, lakini serikali ikapandisha hadi sh. 5,000 wakati malori ilikuwa sh. 25,000 na sasa ni sh. 100,000 kwa tani tano na unatakiwa kupita katika mageti mawili;
"Hivyo kwenda na kurudi huyu wa gari atatakiwa kulipa sh. 400,000 na ikizingatiwa Serengeti tunategemea bidhaa nyingi za viwandani ikiwamo sukari, mabati, sementi (saruji), nondo na vifaa vingi vya ujenzi toka Arusha. Hivyo mtu akitozwa kiasi hicho kikubwa ataweza kuhimili hali hiyo? Ninachoweza kusema ni kwamba huu umekuwa ni mzigo mkubwa kwa wakazi wa Serengeti,"alisema Dkt. Kebwe.
Wakati huo huo, kamati za Bunge zilizoanza jana zinatarajiwa kupitia taarifa na mipango ya utekelezaji katika wizara na taasisi zake na jumla ya miswada sita inatarajiwa kujadiliwa na mingine kuitisha maoni ya wadau.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana na Idara ya Habari, Elimu kwa Umma na Uhusiano wa Kimataifa ilisema kuwa vikao hivyo vitafanyika kwa wiki mbili jijini hapa.
.

No comments:

Post a Comment