Na Yusuph Mussa, Handeni
BAADHI ya Madiwani wa Halmashauri ya Mji
Handeni mkoani Tanga wametaka mkandarasi aliyekuwa anajenga barabara za mji wa
Handeni zenye urefu wa kilomita 11 akamatwe na kufikishwa kwenye vyombo vya
sheria kwa madai amelipwa fedha wakati amejenga chini ya kiwango.
Akizungumza
mwishoni mwa wiki kwenye Baraza la Halmashauri ya Mji Handeni, Diwani wa Kata
ya Vibaoni, Mhandisi Mkusa Nkondo alisema kuna uzembe umefanyika katika kumlipa
mkandarasi huyo fedha za kazi hiyo kwa asilimia 99 wakati hakustahili.
"Mkandarasi
anayejenga barabara za mji wa Handeni hakustahili kulipwa fedha hizo kwa vile
amejenga chini ya kiwango, lakini kibaya zaidi ni kwa nini amekimbilia kulipwa
kwa karibu asilimia 99 ya fedha zote. Maana alikuwa afanye kazi hii kwa sh.
milioni 75 na amelipwa sh. milioni 71.
"Tunaomba
madiwani tupitishe azimio mkandarasi huyu akamatwe ili aweze kufikishwa kwenye
vyombo vya sheria kwa kuchukua fedha ambazo hajazifanyia kazi. Huyu ni mwizi
fedha zimetoka na kazi hajafanya. Ina maana hizi sh. milioni tatu zilizobaki
anaweza kufidia kwa kazi ambayo hajafanya" alisema Mhandisi Nkondo.
Kaimu Mhandisi
wa Halmashauri ya Mji wa Handeni, Joachim Mmbaga alisema alikuwa anaandika
malipo ya mkandarasi huyo kwa shinikizo la Mhandisi wa Ujenzi wa Halmashauri ya
Wilaya ya Handeni aliyefahamika kwa jina moja la Isangura.
"Nilikuwa naandika cheti cha
malipo kwa mkandarasi kwa kushinikizwa. Lakini nilikuwa naambiwa ni haki
mkandarasi huyo kulipwa kwa vile barabara alizokuwa anatakiwa kuzifanyia
ukarabati ni zenye upana wa mita sita, lakini akawa anatengeneza barabara zenye
mita 10, hivyo moramu yake ilikuwa anasambaza zaidi hivyo kuonekana chini ya
kiwango," alisema Mmbaga.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa
Handeni, Thomas Mzinga alisema ni mapema mno kumchukulia hatua za kisheria
mkandarasi huyo hadi hapo watakapopitia taarifa za kazi zake na baada ya hapo
watajua hatua za kuchukua.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri
ya Wilaya ya Handeni Dkt. Khalfany Haule, ambapo halmashauri yake ndiyo
iliingia mkataba wa kutengeneza barabara hizo kwa kiwango cha changarawe,
alisema ofisi yake ni lazima ifuatilie suala hilo na baada ya kupata majibu
watawajulisha madiwani na wajumbe wa baraza hilo.
Akizungumza kwa simu na mwandishi wa
habari hizi akiwa jijini Dar es Salaam, mkandarasi wa kampuni iliyojenga
barabara hizo ya Summer Tec Ltd aliyejitambulisha kwa jina moja la Robert
alisema malipo aliyopewa ni halali na yupo tayari kuitwa na kuhojiwa.
"Mimi nimefanya kazi kwa mujibu wa
sheria na inajulikana wazi barabara niliyokuwa najenga upana wake uliongezeka
karibu mita nne, hivyo kufanya kazi kuwa ngumu, lakini nilifanya kwa ufanisi,
ila kwa vile sijakabidhi kama kuna sehemu itakuwa na kasoro
nitarekebisha," alisema Robert.
Naye Mhandisi Isangura akizungumza kwa
njia ya simu na mwandishi wa habari hizi baada ya kuhamishwa kwenye wilaya
hiyo, alisema hakumshinikiza Mmbaga kuidhinisha malipo ya mkandarasi, bali
walikuwa wanalipa baada ya kujihakikishia kuwa kiwango kilichotengenezwa
kinastahili malipo.
No comments:
Post a Comment