02 August 2013

MEATU WALILIA VIPIMO VYA DAMU



 Na Suleiman Abeid, Meatu
BARAZA la madiwani katika halmashauri ya Wilaya ya Meatu Mkoa wa Simiyu limemwagiza mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, John Wanga kufanya kila linalowezekana ili kuwezesha kununuliwa kwa kipimo cha kupimia sampuli za damu (CD.4) katika hospitali ya wilaya.

Agizo hilo limetolewa juzi na madiwani wakati wa kikao chao cha kufunga mwaka wa fedha ambapo walishitushwa na taarifa iliyotolewa katika kikao hicho na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudhibiti UKIMWI kwamba hospitali ya wilaya haina kifaa cha kupimia CD.4 na hulazimika kupeleka kupima sampuli za damu wilayani Kishapu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya UKIMWI, Basu Kayungilo, mashine ya kupimia CD.4 katika hospitali ya Wilaya ya Meatu iliharibika kipindi kirefu kilichopita ambapo hivi sasa uongozi wa hospitali hiyo hulazimika kupeleka sampuli za damu wilayani Kishapu kwa ajili ya upimaji.
Taarifa hiyo ilifafanua kuwa tatizo lililochangia mashine hiyo kutofanyiwa matengenezo mapema ni ukosefu wa 'spea' zake na kwamba hata hivyo kazi ya ukarabati hupaswa kufanywa na wazabuni waliofunga mkataba na wizara ya afya hali ambayo huchukua muda mrefu kwa kazi kufanyika.
"Mheshimiwa mwenyekiti wilaya yetu hivi sasa inalazimika kupeleka sampuli za damu wilaya ya jirani ya Kishapu kwa ajili ya upimaji ili kuhakikisha damu inayotumika kwa wagonjwa ni damu salama, hali hii ni kutokana na mashine yetu ya CD.4 katika hospitali ya wilaya kuharibika kwa muda mrefu sasa."
"Hali hii ni hatari kwa usalama wa wakazi wetu, hata hivyo urasimu wa wizara ndiyo uliochangia mashine hiyo isikarabatiwe mapema, japokuwa tumeahidiwa kwamba tayari fedha zimepatikana kiasi cha shilingi milioni nne na mwezi ujao kazi ya ukarabati inaweza kuwa imekamilika," alieleza Kayungilo.
Hata hivyo pamoja na taarifa ya mwenyekiti huyo madiwani hao kwa kauli moja waliagiza kununuliwa kwa mashine mpya badala ya kutegemea mbovu na kumwagiza mkurugenzi kufanya chini juu ili mashine hiyo iweze kununuliwa mapema.
Akijibu agizo hilo, mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Wanga alisema suala la kipimo cha damu salama katika hospitali ya wilaya ni la muhimu na kwamba atawasiliana na Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) ili kuanza mchakato wa kupata mashine mpya ya CD.4 hivi karibuni.
Kwa upande mwingine madiwani hao waliagiza kufanyika kwa ukarabati wa vifaa vyote vya upimaji vilivyopo katika hospitali hiyo, vituo vya afya na zahanati ili viweze kufanya kazi kama kawaida kwa lengo la kuwaondolea kero wakazi wa wilaya hiyo kuhangaika katika vituo vya watu binafsi

No comments:

Post a Comment