12 August 2013

JELA KWA KUMTAPELI MGANGA WA KIENYEJI



 Na Said Hauni, Lindi
MAHAKAMA ya Mwanzo Mtama iliyopo Mkoa wa Lindi imemhukumu mkazi wa mtaa wa Shekhe Badi,katika Halmashauri ya Manispaa ya Lindi,Said Abdallah (21) kifungo cha mwaka mmoja gerezani, baada ya kupatikana na kosa la kumtapeli mganga wa Jadi
. Hukumu hiyo ilitolewa hivi karibuni na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama hiyo,Hamisi Katumba baada kuridhishwa na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka.
Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo,Hakimu alimuuliza mshtakiwa kama ana sababu za msingi ili mahakama hiyo,isimpe adhabu kali ambapo aliomba asamehewe,kwani ni mkosaji wa mara ya kwanza na kwamba alilazimika kufanya hivyo kutokana na hali ngumu ya maisha inayomkabili.
Hakimu Katumba akitoa hukumu katika kesi hiyo,alisema hakubaliani na utetezi huo,kwani kazi si ya kuajiriwa pekee,kwani ardhi ipo angeweza kuitumia kwa kazi ya uzalishaji mali mashambani,hivyo akamhukumu kifungo cha mwaka mmoja gerezani ili iwe fundisho kwa wengine.
Awali, ilidaiwa mahakamani hapo kuwa, Julai 21 mwaka huu,kati ya saa 5 na 6 mchana,huko katika Kijiji cha Kilimahewa,Lindi vijijini mshtakiwa akiwa na wenzake watatu,walifika nyumbani kwa mlalamikaji Hadija Bakari Mtondo na kumtapeli kwa kumchukulia shahada ya kupigia kura na fedha taslimu sh. 30,000.
Imeelezwa pia kuwa fedha na shahada hiyo aliichukua kwa madai ya kumtengenezea kitambulisho kinachomtambulisha kazi yake ya uganga wa kienyeji anaoufanya. Mlalamikaji Hadija Bakari Mtondo akizungumza na gazeti hili nje ya mahakama hiyo, alisema amefarijika na hukumu iliyotolewa dhidi ya mshtakiwa wake, licha kukosa shahada na fedha zake.

No comments:

Post a Comment