12 August 2013

KAGAME AMETUMWA KUCHOKOZA TANZANIA?




 HOTUBA ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete ya mwisho wa mwezi Julai inaendelea kujadiliwa na watu katika maeneo yote kwa kadri ya upeo wanavyoiona.Hoja hii ya uchokozi wa Rais Paul Kagame wa Rwanda, kimtazamo inategemewa kujadiliwa na kutafakari kwa kina. Tabia aliyoionyesha Rais Kagame kwa upande wangu imenikasirisha kwa sababu kauli zake na za Serikali yake inachochea uvunjifu wa amani na utulivu katika nchi za Maziwa Makuu
. Na hili ni kama mwendelezo wa matendo yake, kwa sababu upo ushahidi ya kwamba, nchi yake ya Rwanda inaajiri watu wa kujiunga na wapiganaji wa kundi la M23 ili wapigane na majeshi ya Serikali halali ya Jamhuri Kidemokrasia ya Kongo.Katika mapigano yanayoendelea Mashariki mwa nchi hiyo mpaka sasa watu zaidi ya 800,000 hawana maeneo ya kuishi na wanahangaika hovyo kutokana na mapigano hayo.
Inaaminika Rais Kagame ndiye Amiri Jeshi Mkuu wa wapiganaji wa kundi la M23.
Hili la kuichokoza Tanzania, ni sawa na volcano inayotikisa chini kwa chini na inaweza kulipuka wakati wowote.Matusi, kejeli anazofanya Rais Kagame, sio za bahati mbaya, anajua anafanya nini na wala si kwamba hakujua maana ya ushauri wa Rais Kikwete.
Inavyoonekana akiwa Amiri Jeshi wa majeshi ya M23 anayowasaidia, amechukizwa na hatua ya Tanzania ya kupeleka askari kulinda amani huko mashariki ya Kongo.Tabia anayoonyesha Rais Kagame haipishani sana na ile ya marehemu Dikteta Idd Amini Dada wa Uganda. Bila shaka Rais Kagame ana ulevi wa madaraka na hii jeuri na kiburi anachoendelea nacho hajui athari zake.
Rais Kagame inaonekana kuwa ni mwenye tamaa na mbinafsi na hana ari ya kujenga umoja wa Afrika na kama atakuwa na ari hiyo atakuwa amepotea.
Hana hata mkakati wa kutufikisha ama tufikie lengo hilo lililoasisiwa miaka mingi iliyopita na wazee wetu wa Afrika kama vile Julius Nyerere, Patrice Lumumba, Sekouw Toure, Ahmed Benbela, Tafawa Balewa nk.
Wakati Kagame anafanya upuuzi huu tumebakiza siku chache kusherehekea siku ya amani duniani. Nchi za Afrika zikiwa sehemu ya jumuia pana duniani, tutaungana na Mataifa mengine Septemba 21 kuadhimisha siku hiyo.
Na hili ni azimio linalotokana na wakuu wa Serikali za nchi wanachama wa Umoja wa Afrika uliotolewa Tripoli nchini Libya Agosti 31, 2009, iliyoenda sambamba na kauli mbiu ya “Make peace happen” yaani fanya amani iwepo. Lengo lilikuwa ni kudumisha amani.
Mwenzetu Kagame hayataki hayo, anataka “fanye vita itokee” “let the war happen” sisi tunamshangaa. Sijui kama Kagame amesahau yaliyotokea nchini mwake. Matokeo ya vita na mamilioni ya watu wasio na hatia kupoteza maisha yao, kujeruhiwa hususan watoto na wanawake wajawazito ambao wanataabika sana.
Vita inaharibu miundombinu ambayo Serikali zetu imejitahidi kuzijenga kwa fedha nyingi na hata kwa mikopo toka nje. Vita inavuruga sana uchumi na maendeleo ya nchi. Fedha zote zilizokuwa zielekezwe kwenye huduma muhimu za jamii kama afya, elimu, maji nk. Baadala yake zinaelekezwa kwenye ununuaji wa silaha.
Na kwa sababu Kagame hajui kwamba tutakakaonunua silaha hizo ni kwa hao hao waliomsukuma atuchokoze yeye anawasikiliza. Rais Kagame atambue kwamba moja ya mbinu na silaha kubwa inayotumika na wakubwa hao ni kutugawa ili Afrika idhoofike isiwe na nguvu.
Lengo lao ni kutafuta fursa ili kuzifikia rasilimali kwa ajili ya kujiimarisha kiuchumi. Rasilimali zetu, zikiwemo ardhi, gesi, mafuta, uranium ni bidhaa adimu sana duniani lakini Rais Kagame halielewi hilo.
Kwa taaluma yake ya kijeshi, Rais Jakaya Mrisho Kikwete ametufungua masikio Watanzania kwamba, siri ya vita siku zote ni kutomdharau adui. Kwa maana nyingine ameturudisha kwenye maandiko matakatifu ya Biblia juu ya vita ya Goliathi na Daudi.
Goliath lilikuwa jitu kubwa lenye miraba minne, lakini lilibwagwa na mtu mdogo Daudi. Udogo wa nchi ya Rwanda tusiudharau hatufahamu Rais Kagame anafanya jeuri hiyo kwa maandalizi yapi.
Vita ni kuwahi ndio sababu katika hotuba yake Rais Kikwete alisema “Amesikia mengi sana yanayozungumzwa na kudaiwa kupangwa na kufanywa na Serikali ya Rwanda dhidi yake yeye mwenyewe na nchi ya Tanzania. Kwa hiyo kamwe hawezi kuyapuuza ingawa hapendi kuyaamini moja kwa moja”
Hii maana yake nini? Maana yake ni kwamba tuwe na hadhari. Anatukumbusha yale ya Nduli Idd Amini, naye alianzisha chokochoko zinazofanana sawa na hizi za Kagame, hivyo inawezekana kukawa na ukweli wa kauli za Kagame.
Kuna haja ya kuchukua hatua za dharura na haraka za kuilinda nchi yetu. Hili sio suala la hiari, ni jambo la lazima ili kuja kuhimili uvamizi wowote endapo utatokea.
Labda nitoe ushauri kwa Serikali yetu kwamba, ianze kuandaa mazingira ya kiulinzi yatakayotokana na uvamizi wowote, kwani “HATUIJUI SIKU HATA SAA.” Turejeshe kwa haraka na kwa msisitizo mafunzo ya mgambo. Liwe ni suala la kufa na kupona, lifanywe na kupangwa kimkakati na kwa malengo.
Ikumbukwe kwamba, vijana wale waliohitimu mgambo miaka ya 1970 ndio baadaye lilikuja kuwa jeshi la akiba na ndilo tulilitumia katika vita ile dhidi ya Idd Amini. Vijana wale wamekuwa watu wazima sasa na wengine walijiunga na Jeshi la Wananchi wa Tanzania.
Kwa sasa tuna upungufu mkubwa wa jeshi la akiba, kwani baada ya vita ile tumezembea katika mafunzo ya mgambo. Vijana karibu wote waliopo leo hawajapitia jeshi.
Tuwaandae vijana sasa ili waanze kujenga uzalendo miongoni mwao, kuvunja matabaka ya itikadi za kisiasa zilizowagawa ili wabaki kitu kimoja, nia ni kuilinda Tanzania kama mboni ya jicho. Kila Mtanzania mahali alipo aanze kujitayarisha ili kujitoa mhanga endapo litatokea lolote.
Serikali nayo kwa upande wake iangalie matumizi yasiyo ya lazima yanayohitaji fedha za kigeni. Tuwe na akiba ya kutosha.
Tanzania ni nchi inayosifika kuwa na amani, utulivu, demokrasia, utawala bora na haki za kibinadamu. Tanzania na Rwanda zina uhusiano wa undugu, na umeenda mbali zaidi, kuwa na uhusiano wa diplomasia ya uchumi kwani wote tuko katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na (SADC) nchi ya Kusini mwa Afrika, kwa hiyo matokeo yoyote ya vita sote sisi tutakuwa tumeathirika na jumuiya hizo nazo zitaathirika.
Hata hivyo Rais Kagame anapaswa kuelewa kuwa mapenzi kwa nchi ya Rwanda yatapungua, lakini undugu wetu hautaisha.
Vilevile masuala haya hayataki ubabe wala jazba bali ayaangalie kwa uzito kuhusiana na hoja za Rais Kikwete, kwa manufaa ya nchi zetu na za maziwa makuu, sio leo tu bali kwa muda mrefu.
Rais Kagame alitoa lugha zisizostahili dhidi ya Rais Kikwete katika sherehe ya kuhitimu mafunzo ya kijeshi ya maofisa 45 wa jeshi lake Julai mwaka huu, ambapo alisema ushauri wa kufanya mazungumzo na waasi wa FDLR ni ujinga na haupo katika historia ya Wanyarwanda.
“Nilinyamaza kimya kwa sababu sikupenda kusikiliza ushauri kuhusu FDLR, kwa sababu nafikiri ni upuuzi ulioambatana na ujinga. Hatuwezi kuacha maisha yetu kama Wanyarwanda tunavyoishi sasa. Ushauri wa Kikwete ni sawa na kucheza na makaburi ya watu wengi ambao ni ndugu zetu,” alisema Kagame.
Katika hotuba ya Rais Kikwete alisema uhusiano wa Tanzania na Rwanda unapitia katika wakati mgumu na mtikisiko, baada ya yeye kutoa ushauri kwa Serikali ya Rwanda kuzungumza na mahasimu wao na kwamba hilo linadhihirika katika kauli zinazotolewa na viongozi wa Rwanda.
“Napenda kuwahakikishia Watanzania wenzangu na ndugu zetu wa Rwanda kuwa mimi, Serikali ninayoiongoza na wananchi wa Tanzania, tunapenda kuwa na uhusiano mzuri na ushirikiano wa karibu na Rwanda kama ilivyo kwa nchi zote jirani,” alisema Rais Kikwete.
Alisema nchi hizo ni jirani na kila moja inamuhitaji mwenzake, hivyo lazima ziwe na uhusiano mwema na ushirikiano mzuri.
“Nasisitiza kuwa mimi na Serikali ninayoiongoza tutakuwa wa mwisho kufanya kitendo au vitendo vibaya dhidi ya Rwanda au nchi yoyote jirani au yoyote duniani. Hatuna sababu ya kufanya hivyo, kwani ni mambo ambayo hayana tija wala masilahi kwetu,” alisema.
Alisema nchi hizo mbili zimekuwa zikijihusisha na mambo ya kukuza na kujenga ujirani mwema, kusisitiza kwamba hiyo ni moja ya nguzo kuu ya Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania

No comments:

Post a Comment