Na Amina Athumani
SHIRIKISHO la Kimataifa la Riadha
(IAAF), limezitaka serikali kuacha kuingilia masuala ya mchezo huo na kuachia
vyama husika kuisimamia na wao wakibaki kama wadhamini.Hatua kama hiyo pia hutumiwa na
Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), ambalo halitaki wanachama
wake kuingiliwa na serikali.
Rai hiyo imetolewa katika Mkutano Mkuu
wa marais wa mchezo huo Duniani uliofanyika Moscow, Urusi kabla ya kuanza
kutimua vumbi mashindano ya Dunia, ambayo yanaendelea nchini humo na
kuhudhuriwa na washiriki 206.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Rais wa
Chama cha Riadha Tanzania (RT) Antony Mtaka, alisema mkutano huo ulijadili
masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na hilo ikiwa ni kwa manufaa ya mchezo wa
raidha kwa kila nchi.
Alisema pia kulijadiliwa utumiaji wa
dawa za kuongeza nguvu, ambazo zimekuwa ni gumzo katika maendelo ya michezo,
ambapo wanariadha wengi wamekuwa wakibainika kutumia dawa za kuongeza nguvu na
kuweza kushinda katika mshindano mbalimbali.
Rais huyo alisema, kutokana na maagizo
hayo, RT imejipanga kusimamia kila nyanja kuhakikisha mchezo huo unasimamiwa
ipasavyo.
Mtaka alielezea mikakati mbalimbali
waliyoiweka katika kuhakikisha mchezo huo unapiga hatua kubwa hapa nchini ikiwa
ni pamoja na kuandaa katiba ya RT, itakayobeba mambo ya msingi ya chama hicho.
Alisema pia hawakusita kuomba msaada wa
kuletewa walimu wa kimataifa, watakaoweza kuwafunza wachezaji wa hapa nyumbani
na katika barua yao wamemuomba, Rais Jakaya Kikwete kuwaletea makocha kutoka
Jamaica wakiamini wana uwezo mkubwa wa kufundisha wanariadha.
Rais huyo alisema mikakati iliyopo sasa
ni kuhakikisha wanaendeleza vipaji vya riadha vilivyovumbuliwa katika
mashindano ya UMISSETA na UMITASHUMTA, hususani vijana waliopata nafasi ya
kushiriki mashindano ya Afrika Mashariki.
Alisema ipo mipango mizuri ya
kuhakikisha vijana hao, wanapatiwa mafunzo katika vituo vya michezo na tayari
wameshaomba kupunguziwa ada ya kupeleka vijana katika kituo cha michezo,
kilichopo nchini Kenya.
No comments:
Post a Comment