12 August 2013

CUF YAMKALIA KOONI MBUNGE CCM



 Na Mashaka Mhando, Korogwe
CHAMA Cha Wananchi (CUF) wilayani Korogwe kimetamba kushinda ubunge katika jimbo la Korogwe Mjini, kutokana na madai kwamba mbunge aliyepo sasa, Yusuph Nassir kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), kushindwa kukidhi matarajio ya wananchi wa jimbo hilo tangu achaguliwe mwaka 2010
. Akizungumza na waandishi wa habari mjini humo, Kaimu Katibu wa CUF wilaya ya Korogwe, Ibrahim Abdillahi alisema kuwa kitendo cha mbunge huyo kulikimbia jimbo lake kwa kipindi kirefu tangu achaguliwe kinawapa nafasi ya kujinadi kwa wananchi kisha kushinda kirahisi mwaka 2015 kwa kuwa wananchi wa jimbo hilo, wana kiu kubwa ya maendeleo hasa kasi aliyokuwa nayo Mkuu wa wilaya hiyo, Mrisho Gambo.
"Wananchi wa Korogwe mjini hatuna wa kutusemea sio bungeni wala kwenye mikutano ya hadhara ya viongozi wa Serikali wanapokuja Korogwe, mbunge wetu hatujui nini kimempata kwa sasa...Haonekani kwenye mikutano yake hata ile ya viongozi wa kiserikali wanaokuja kutembelea jimbo lake," alisema Ibrahim.
Alisema mbunge huyo tangu amechaguliwa kuwa mbunge mwaka 2010 alipomwangusha, Joel Bendera (sasa Mkuu wa Mkoa Morogoro), hajawahi kufanya mkutano wowote na wananchi wa jimbo lake hatua ambayo kisiasa wanaielezea kama kukosa dira na mwelekeo wa kugombea tena katika kipindi kijacho kwa kuwa atakosa la kuwaeleza wananchi na wakamkubalia.
Akitoa sababu za kueleza suala hilo Ibrahim ambaye pia aliwahi kuwa Mkurugenzi wa Haki za Binadamu wilayani hapa kupitia chama hicho, alisema kuwa hivi karibuni Mkuu wa Mkoa wa Tanga Luteni (mstaafu) Chiku Gallawa alifanya ziara wilayani hapo lakini mbunge huyo hakuwepo wala kushiriki ziara yake hatua ambayo wananchi wanashindwa kuelewa ni nini kimempata.
Alisema hivi karibuni halmashauri ya mji ilitenga viwanja takribani 2000 na kuviuza kati ya kiasi cha shilingi milioni 1.8 hadi shilingi milioni 5, lakini wananchi wa jimbo hilo hawakuwa na sehemu ya kupeleka malalamiko kwa vile kiasi hicho ni kikubwa na kwamba wenye uwezo wa kununua ni wageni tu na wananchi wa Korogwe hawawezi kiasi hicho.
Ibrahim alisema endapo wangekuwa na mbunge angeweza kuwatetea kuonesha kwamba wananchi wa mji wa Korogwe hawana kipato kinachoweza kuwafanya waweze kununua kiwanja cha bei hiyo hivyo, ilikuwa ni sehemu nzuri kwa mwakilishi wao kujenga hoja na kuwatetea wananchi wake.
Hata hivyo akizungumza na mwandishi wa habari kuhusiana na madai hayo, Mbunge huyo alisema kuwa malalamiko yanayotolewa dhidi yake hayana ukweli wowote bali yana lengo la kumchonganisha na wananchi huku akidai kukosekana kwake kwenye ziara ya Mkuu wa Mkoa inatokana na kuhudhuria katika mkutano wa wabunge Jumuiya ya Madola uliofanyika kwa siku 10 tangu Julai 13 hadi 27, nchini Namibia.
"Kwanza huyo Ibrahim ni ndugu yangu ninamwelewa vizuri hao watu wa CUF hawamjui historia yake hadi wakampa huo ukatibu wa wilaya na hawatashinda wakiwa na katibu huyo...na suala la kutokuwepo kwenye ziara ya RC mimi niliongoza ujumbe wa mkutano wa Jumuiya ya Madola tulikuwa Namibia kwa siku 10," alisema Nassir.
Kuhusu suala la viwanja alisema bei iliyopangwa na Halmashauri ya Mji ni rahisi kiasi kwamba mwananchi yeyote anaweza kununua na kumiliki kiwanja tofauti na maeneo mengine ya nchi wanavyouza ambayo ni bei kubwa kiasi cha wananchi kushindwa lakini hata hivyo alisema endapo mkazi wa Korogwe anataka kiwanja katika eneo la mji anaweza kwenda Kwamsisi na atanunua kiwanja kwa bei ya sh. 200,000.

No comments:

Post a Comment