22 August 2013

CHINA YAWEZESHA UKUAJI WA UCHUMI BARANI AFRIKA



MAPINDUZI makubwa ya kiuchumi yaliyofanywa kimahiri na Jamhuri ya Watu wa China katika miaka ya 80 yamesaidia kuziwezesha nchi nyingi zinazoendelea duniani kupiga hatua zaidi ya maendeleo, kiuchumi na ustawi wa jamii.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi alisema hayo katika tafrija maalum aliyomuandalia Balozi Mdogo wa Jamuhuri ya Watu wa China hapa Zanzibar Balozi Chem Qiman kwa ajili ya kumuaga rasmi akikaribia kumaliza muda wake wa utumishi wa Kidiplomasia hapa Zanzibar.
Tafrija hiyo mahsusi iliyoshirikisha pia baadhi ya Mawaziri, Makatibu Wakuu wa Serikali na baadhi ya watendaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilifanyika katika Hoteli ya Serena Inn iliyopo Shangani Mjini Zanzibar na kuambatana na muziki laini uliokuwa ukitumbuizwa na Kikundi maarufu cha kizazi kipya cha Akheri Zamani.
Balozi Seif alisema mapinduzi hayo ya kiuchumi ya China yametoa fursa kwa watendaji mbalimbali wa taasisi za umma na hata zile binafsi sambamba na jumuiya za uzalishaji katika mataifa machanga kupata taaluma tofauti nchini humo.
Balozi Seif alifahamisha kwamba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imelazimika kumpa heshima kubwa Balozi Chen kutokana na mchango wake mkubwa uliosaidia kuratibu uhusiano wa pande hizo mbili hasa katika masuala ya taaluma,maendeleo na mwelekeo wa miradi ya uwekezaji.
Akitoa shukrani zake Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Watu wa China Chen Qiman amewapongeza Viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na wananchi wake kwa ushirikiano waliompa wakati akitekeleza majukumu aliyopangiwa na Taifa lake, ambapo umemwezesha kufanya kazi zake kwa ufanisi na umahiri mkubwa wa hali ya juu.

No comments:

Post a Comment