15 August 2013

CCM YANUSURU MADIWANI WALIOFUKUZWA BUKOBA



 Na Leah Daudi
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimetengua uamuzi uliotolewa na Halmashauri Kuu ya Mkoa wa Kagera kuwavua udiwani madiwani nane wa chama hicho uliofikiwa juzi mkoani humo hadi itakapoamuliwa vinginevyo na Kamati Kuu ya Halmashauri ya Taifa itakayokutana
.Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa Itikadi na Uenezi ya CCM, Nape Nnauye, alisema madiwani hao waliokuwa wamesimamishwa kazi wanatakiwa kuendelea na shughuli zao kama kawaida wakisubiri uamuzi wa kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa kitakachofanyika Agosti 23, mwaka huu, mkoani Dodoma.
Alisema kikao hicho pamoja na mambo mengine kitapitia uamuzi huo wa Halmashauri Kuu ya CCM mkoani Kagera.Nape alisema utaratibu wa kutoa adhabu kwa viongozi wa CCM walio kwenye vyombo vya dola hasa wabunge na madiwani uamuzi wa Halmashauri Kuu ya Mkoa sio wa mwisho.
Alifafanua kuwa uamuzi unatakiwa kupata baraka za Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa na ndio utekelezwe. Alisisitiza kuwa uamuzi ulitakiwa kupitia katika Baraza la Kamati Kuu ya Halmashauri ya Taifa ndipo uchukuliwe na sio vinginevyo.
Alisema tayari wamepokea barua za kukata rufaa kutoka kwa madiwani hao za kukata rufaa kupinga uamuzi huo wa Halmashauri Kuu ya Mkoa kwa hoja kwamba taratibu zilikiukwa wakati wa kufikia uamuzi huo.
Juzi Halmashauri Kuu ya CCM ilitangaza kuwafukuza uanachama madiwani hao Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Bukoba ambaye pia ni Diwani wa Kashai, Yusuph Ngaiza, Alexander Ngalinda (Buhembe), Samuel Ruhangisa (Kitendaguro), Dauda Kalumuna (Ijuganyondo), Deus Mutakyahwa (Nyanga) na Robert Katunzi (Hamugembe).Wengine Richard Gasper (Mihembeni) Mulundi Baduru Kichwabuta (Viti maalum).

No comments:

Post a Comment