01 August 2013

CCM YAIPONGEZA SERIKALI KUKUBALI KUJADILI TOZO



 Na Eckland Mwaffisi
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimeipongeza Serikali kwa kusikiliza kilio chao na kukubali kujadili namna ya kusitisha tozo ya sh. 1,000 kila mwezi kwa kila laini ya simu iliyopaswa kulipwa na watumiaji wa simu za mkononi.

Pongezi hizo zimetolewa jana na Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi wa CCM, Bw. Nape Nnauye wakati akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu akiwa mkoani Kigoma na kusisitiza kuwa, chama hicho kiliitaka Serikali iangalie njia nyingine ya kupata vyanzo vya mapato badala ya kodi hiyo.
Alisema, kwa kuwa Serikali imeamua kulirudisha suala hilo bungeni, CCM inatoa wito kwa wabunge ambao wengi wao wanatoka chama tawala, kulijadili suala hilo kwa makini na kuishauri Serikali vyanzo vingine vya mapato.
“CCM ni chama makini kinachowajali wananchi ndio maana tulianza kupiga kelele za kupinga tozo hii ambayo ingewaumiza Watanzania...leo (jana) hii Waziri wa Fedha, William Mgimwa ametangaza msimamo wa Serikali ambao umezingatia agizo alilotoa kiongozi wa nchi Rais Jakaya Kikwete.
“Katika agizo lake, Rais Kikwete ameitaka Wizara ya Fedha ikutane na wadau ili kuangalia namna nyingine ya kupata vyanzo vya mapato badala ya kodi hii,” alisema Bw. Nnauye.
Hata hivyo juzi Waziri Mgimwa alisema suala hilo litafikishwa bungeni mjini Dodoma Agosti mwaka huu na kumalizwa kisheria baada ya Rais Kikwete kuitaka Wizara hiyo, Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia na kampuni za simu kumaliza utata uliojitokeza juu ya kodi hiyo.
Awali Umoja wa Wamiliki wa Kampuni za Simu nchini (MOAT), ulitoa maoni yao ukitaka kodi hiyo ifutwe baada ya kulalamikiwa na wadau wa sekta ya mawasiliano.
Mbali ya MOAT, baadhi ya viongozi wa Serikali, wabunge na wananchi nao walipinga kodi hiyo wakidai itaongeza ugumu wa maisha kwa watumiaji wa simu za mkononi hasa wa kipato cha chini.  

No comments:

Post a Comment