02 August 2013

BALOZI IDD ATAKA UFANISI TAASISI ZA FEDHA



Na Mwajuma Juma


 U ONGOZI wa Benki ya Posta Tanzania umetakiwa kuzidisha juhudi za kufungua matawi yake hasa vijijini ili kuondoa urasimu kwa wateja wake wanaolazimika kufuata huduma hiyo katika maeneo ya mijini.Wito huo ulitolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi mara baada ya futari ya pamoja iliyoandaliwa na benki hiyo Kilimani mjini Unguja
. Balozi Seif alisema kuwa wakati umefika kwa benki hiyo kuzidisha ushindani wa huduma zake hasa kwa vile kumekuwa na ongezeko kubwa kwa huduma za kifedha kitaifa na kimataifa ndani ya mfumo wa Mtandao wa Mawasiliano.Alisema wananchi walio wengi katika baadhi ya maeneo hasa vijijini bado wanaendelea kupata usumbufu wa huduma za kibenki wakati wanapotaka kuhifadhi fedha zao mara wauzapo mazao na bidhaa wanazozalisha mashambani.
"Ongezeko la huduma za kibenki kwa ufunguzi zaidi wa matawi kwenye makazi yao utatoa fursa zaidi kwa wakulima hao muda mwingi kushughulikia uzalishaji wa miradi yao na kuongeza mapato sambamba na kupunguza umaskini," alisema.Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliupongeza uongozi na wafanyakazi wa Benki ya Posta Tanzania kwa juhudi zao za kutoa huduma za Kibenki katika maeneo tofauti hapa nchini wakielewa kwamba mteja kwao ni mfalme.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Saba Saba Mushingi alisema yapo mafanikio makubwa ndani ya benki hiyo tangu kuanzishwa kwake mnamo mwaka 1927 na hivi sasa inajitegemea kwa zaidi ya miaka 12 baada ya mabadiliko ya kisera yaliyotokea mwaka 2001.
Mkurugenzi huyo aliwahakikishia wananchi na wateja wao kwamba Uongozi wa Benki hiyo umezingatia umuhimu wa kuongeza huduma zake na tayari hivi sasa yapo matawi yasiyopungua 15 ya benki hiyo likiwemo pia lile la Chake Chake Kisiwani Pemba.
Mapema Meneja wa Benki ya Posta Tawi la Zanzibar ambalo ndiyo mwenyeji wa hafla hiyo, Hassan Mohd aliwahakikishia wananchi kuendelea kupata huduma za kibenki katika kiwango kinachoridhisha.

No comments:

Post a Comment