22 July 2013

WANAWAKE WALILIA MIRATHI KATIBA MPYA



BAADHI ya wanawake katika Kata ya Pasua, Manispaa ya Moshi wametaka mabaraza ya katiba kuweka vipengele vinavyoainisha mirathi, haki za wanandoa na watoto mara baada ya ndoa kuvunjika na mmoja au wote wanapofariki.Wanawake hao Mwanvita Kishe na Lillian Mwendani walisema hayo katika mdahalo wa usawa wa kijinsia ulioandaliwa na asasi ya mazingira mkoani Kilimanjaro (KENOT) kwa ufadhili wa The Foundation For Civil Society na kufanyika mjini humo.

Walisema ombi hilo linatokana na unyanyasaji wanaopata wanawake, watoto wanaozaliwa kabla, baada ya ndoa kuvunjika na wale wanaotelekezwa kutokana na matukio hayo kukithiri katika siku za hivi karibuni."Kwa kuwa katiba ndiyo sheria mama ipo haja kuainisha baadhi ya masuala ambayo yamekuwa kikwazo kwa wanawake wajane na watoto wote bila kujali amezaliwa kabla au baada ya ndoa," alisema Massawe
Alisema kuna baadhi ya sheria zikiwemo za ustawi wa jamii na zile za ndoa ambazo hazitoi haki sawa baada ya watu kuchuma kwa pamoja na badala yake wanawake wamekuwa wakiteseka na watoto wanaoachiwa.Awali akichangia katika mdahalo huo Ustadhi Marimbo Mmbaga aliziomba asasi hizo na viongozi wengine wa dini kusaidia kutoa elimu sahihi juu ya usawa wa kijinsia ili kuepusha upotoshaji unaofanyika.
Alisema usawa wa kijinsi unapaswa kuandamana na kusaidiana katika majukumu ya kila siku, haki na wajibu katika jamii na sio kama inavyotafsiriwa na baadhi ya watu na kukataa kufanya kazi.Kwa upande wake Mwenyekiti wa KENOT, Rodrick Maimu alisema suala la haki sawa linahitaji elimu na muda zaidi wa kuirekebisha jamii kwani kutokana na mfumo wa hapo awali mwanamke alionekana kutokuwa na thamani kabisa

No comments:

Post a Comment