Na Said Hauni, Lindi
WANANCHI wa Kijiji cha Milola Mashariki
Wilaya ya Lindi wameilalamikia kamati mbili zilizopewa kazi ya kukusanya
maduhuli yatokanayo na michango na mauzo ya maji katika kipindi cha miaka
miwili sasa.Madai hayo yametolewa jana na wananchi
hao, walipokuwa wakiwasilisha kero zao mbalimbali zinazowakabili kwa Mkuu wa
Mkoa huo, Ludovick Mwananzila, katika mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja
vya mahakama ya mwanzo.
Wananchi hao wamelazimika kutoa kilio
hicho kutokana na kuwepo kwa madai kwamba wakazi hao hawataki kushiriki kazi za
kujiletea maendeleo yakiwemo kuchimba mitaro kwa ajili ya kulaza mabomba ya
maji kutoka kijiji cha Namtanga hadi kijijini hapo.Inaelezwa kwamba serikali kupitia
wizara ya maji imetoa jumla ya sh. milioni 100 kwa ajili ya ununuzi wa mabomba
600 ya maji na kuwasilishwa kwenye kata tayari kwa ajili ya kuyalaza kutoka
chanzo cha maji kilichopo Kijiji cha Namtanga hadi Milola.
Akiwasilisha kilio chao kwa niaba ya
wakazi wenzake,Ibrahimu Said Malango,alisema wananchi wa kijiji hicho,
wanalazimika kususia kushiriki shughuli mbalimbali za kujiletea maendeleo yao
kutokana na viongozi wao zikiwemo na kamati mbili zilizopewa kazi ya kukusanya
maduhuli wa ushuru wa maji kutia ndani michango wanayotoa.Malango alidai kwamba kamati ya kwanza
imetia ndani jumla ya sh. milioni 15 na iliyofuata inadaiwa pia kutafuna kiasi
cha sh milioni 16. 8 na kufanya jumla ya maduhuli yaliyotafunwa kufikia sh.
milioni 31.8.
"Katika suala la kuchangia
maendeleo sisi wana Milola tupo mstari wa mbele,tatizo tunakatishwa tamaa na
baadhi ya viongozi wetu..sikufahamu kama ziara yako hii utagusia suala la maji
ningechukuwa risiti zangu uzione," alisema Malango huku akipigiwa makofi
na wananchi waliokuwa wamehudhuria mkutano huo.Malango alisema wananchi walikaa kikao
kupitia taarifa ya mapato na kubaini fedha zilizokusanywa zimetiwatumiwa na
watu aliowaita kuwa ni wajanja wachache huku hakuna hata senti moja iliyotumika
kwa kazi yeyote iliyohusu kusukuma maendeleo ya kata yao.
Alisema mwezi Juni mwaka huu,kamati
nyingine iliyoundwa imefanya tathmini na kupata thamani ya fedha zilizokusanywa
na kamati ya pili na kubaini sh. 16,800,000 zilizokusanywa zimetafunwa na
kamati hiyo yenye wajumbe wanane.
Malango alisema wingi wa mapato
yanayopatikana ndani ya kata yao,yangetosha kubadilisha sura ya kata
yao,ikiwemo hata ununuzi wa mabasi au matrekta ambayo yangewasaidia kwa kazi ya
kusafirisha abiria na kilimo.
Wananchi hao wamesema kutokana na
kushamiri kwa vitendo hivyo vinavyofanywa na baadhi ya viongozi wao,ikiwemo
kamati za maji, zilizochaguliwa vipindi vilivyopita kutokuwa waaminifu
kunawafanya wananchi wakatishwe tamaa ya kushiriki kazi za kujiletea maendeleo
yao.Baada ya kilio hicho, Mkuu wa Mkoa wa
Lindi, Ludovick Mwananzila amewataka viongozi wa serikali wa kijiji hicho,
kuhakikisha wanatumia Sheria na kanuni zilizowekwa za kuwapatia wananchi
taarifa za mapato na matumizi yanayoingia ndani ya kijiji chao ili kuondoa
malalamiko kwa jamii.
"Ebu mwenyekiti wa Serikali ya
kijiji kaa na watendaji wako na mtoe taarifa ya mapato na matumizi ya kijiji
chenu, ili kuondoa malalamiko......, hapa leo wanasema milioni 15 za maji
zimetafunwa kumbe inaweza kuwa ni milioni tano tu sasa ni bora mkaeleza
ukweli," alisema Mwananzila.Pia mkuu huyo wa mkoa amuagiza mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya
wilaya hiyo, Grace Mbaruku, kuunda tume itakayofuatilia madai ya wananchi hao
ili kubaini ukweli wa madai hayo na pale itakapobainika kuwa yana ukweli
achukue hatua kwa wahusika.
No comments:
Post a Comment