26 July 2013

WANANCHI MARA WATAKIWA KUEPUKA UHASAMA



 Na Timothy Itembe, Tarime
MKUU wa Mkoa wa Mara, John Tuppa amewataka wananchi wa mkoa huo kudumisha amani na kutojengeana chuki ambazo zitasababisha uhasama na kusababisha mapigano ya koo na kutaka amani iliyopo sasa wilayani Tarime iendelee kudumishwa. Hayo aliyasema jana mbele ya wananchi wa Kijiji cha Mugabiri wakati wa mazishi ya Mwanajeshi wa Jeshi la Wananchi (JWTZ), Peter Muhiri Werema aliyefariki huko Darfur.

Tuppa alisema kuwa iwapo wananchi wa Mara watavunja amani na kuwa na ubaguzi wa kabila na dini ni kiashirio kuwa siku moja Watanzania wakalindwa na watu wa Mataifa na huenda vikatokea vifo kama kilivyotokea cha mwanajeshi huyo Mtanzania na wenzake aliyefia huko Darfur nchini Sudan wakati akitekeleza majukumu yake ya kazi.
Naye Luteni Dickson Mnubi kutoka kikosi cha 44 KJ Mbalizi Mbeya alikokuwa akifanya kazi marehemu Werema akisoma wasifu wa marehemu alisema kuwa marehemu alizaliwa mwaka 1984 na alijiunga na Jeshi Machi 2007 na katika utumishi wake alihudhuria kozi ya mafunzo ya awali-RTS Makutopora -2007, mafunzo ya askari wa miguu daraja la tatu-44 KJ- 2007, mafunzo ya askari wa miguu daraja la pili- 42 KJ 2008 na kozi ya Polisi Jeshi Daraja la tatu- 832KJ -2010.
Luteni Mnubi alisema kuwa madaraja aliyowahi kuhusika wakati wa utumishi wake alishika madaraka ya polisi jeshi kitengo cha MP Section ambapo pia alitunukiwa medali ya miaka 40 ya JWTZ ya kuthamini mchango wake katika jeshi hadi hapo alipofariki Julai 14 huko Darfur akitekeleza majukumu yake ya kazi.
Kwa upande wake mke wa marehemu Mary Peter (27) alisema kuwa kifo cha mumewe huenda akaishi maisha magumu yeye na watoto wake 3 wa kike aliowaacha kwakuwa mama huyo hakuwa na kazi yoyote ya kufanya alikuwa ni mama wa nyumbani.
"Mume wangu ameniacha na watoto wadogo mwisho wa kuonana naye akiwa hai ilikuwa Februari 7, 2013 kafa bila hata kuniambia chochote mimi mkewe sina kazi sijui nitaishi vipi kwani hata huko Mbeya tulikuwa tunaishi kwenye nyumba za jeshi," anasema mama huyo kwa uchungu.
Mary aliiomba Serikali kumjali yeye na familia yake kwakile alichoeleza kuwa mumewe kafa akiwa kazini tena akitekeleza majukumu ya kazi nje ya nchi yake hivyo yeye na familia yake ni vyema wakalipwa haki stahili za mume wake ili ziwakwamue kimaisha na wala wasiwepo watu wa kuingilia na kunyang'anya mirathi ya mumewe.
.

No comments:

Post a Comment