30 July 2013

WANAFUNZI WAANDAMANA KUPINGA UONGOZI WA SHULE




 Na Lilian Justice, Morogoro

WANAFUNZI 600 wa Sekondari ya Junior S e m i n a r y i l i y o p o Manispaa ya Morogoro wameandamana kutoka shuleni hadi ofisi ya Askofu Mkuu wa Kanisa la Kilutheri Dayosisi ya Morogoro, Jacob Mameo kwa madai ya kutaka kuondolewa kwa mkuu wa shule hiyo Laiser Saningo kutokana na uongozi wake mbovu uliosababisha matokeo mabaya.


Wakizungumza na wanahabari kwa kutokutaja majina yao walisema kuwa ni muda mrefu wamekerwa na uongozi wa shule kiasi ambacho kumechangia shule hiyo kufanya vibaya katika matokeo ya kidato cha nne na sita katika miaka mitatu iliyopita.

Aidha wanafunzi hao walisema kuwa shule hiyo ina matatizo ya upungufu wa vitabu vya biologia na pindi wanapouliza kwa uongozi wa shule wanaambiwa shule inatafuta pesa,ukosefu wa kiu ya taaluma imeshuka kutokana na walimu kutokuwa na mwamko wa kutoa mitihani ya majaribio ya mara kwa mara inayowafanya kufanya vizuri katika mitihani ya mwisho.

"Walimu wetu hawamalizi mitaala kwa muda unaotakiwa hususan vidato vya nne na sita, kutopewa mitihani ili kujifunza hivyo kupelekea matokeo kuzidi kushuka kama yalivyo matokeo ya kidato cha sita 2013 na hii inatokana na walimu hawapewi motisha wa kufundisha," walisema.

Pia walibainisha kuwa wanafunzi wa kidato cha nne walikaa kikao na mkuu wa shule na kumuuliza swali kuhusu mitihani ya ndani na nje lakini walishangazwa na jibu lililotolewa ni kwamba shule haina pesa jambo ambalo linawakatisha tamaa kutokana na ada kubwa inayolipwa na wazazi wao.

Waliongeza kuwa jambo lingine ni kubadilishwa ghafla kwa sheria za shule bila ya maelezo yoyote kutoka kwa uongozi na hivyo kuwa kandamizi na baadhi ya sheria hizo zinawapa mashaka uongozi wa shule unatumia kuficha maovu yao kwa wanafunzi kutokana na wawakilishi katika vikao vya shule ni walimu na sio Serikali ya wanafunzi

Pia walidai kuwa kusikitishwa na walimu kuendeshwa kidikteta na uongozi wa shule na kusababisha baadhi yao kuondoka na kushindwa kusimamia wanafunzi ipasavyo na hatimaye kutafutwa walimu wengine ambao hawana sifa za kufundisha wala za ualimu na kufanya taaluma kuporomoka kila mwaka.

Madai mengine ya wanafunzi hao ni kukosekana kwa dawa katika zahanati ya shule, uchache wa wauguzi, chakula maalumu cha wagonjwa, vitanda vichache vya wagonjwa, kutokuwepo kwa madaktari siku za Jumapili na Jumamosi, hali hii inachangia kwa kiasi kikubwa afya za wanafunzi kuwa matatani pindi kunapotokea magonjwa ya mlipuko.

Kwa upande wake Askofu wa Kanisa la Kilutheri Dayosisi ya Morogoro, Jacob Mameo akizungumza na wanafunzi hao katika Kanisa la Mji Mpya mjini humo alisema kuwa maandamano waliyofanya wanafunzi hao wametumia njia halali ya kudai haki zao pasipo kufanya vurugu wala kuharibu mali za shule na umma kwa ujumla.

Askofu Mameo alisema kuwa bodi ya shule itakaa na kutatua kero hizo za wanafunzi mapema ili kuwafanya kuweza kuendelea na masomo yao kwa kufuata taratibu na sheria za shule zilizowekwa zikiongozwa na Kanisa hilo.

Mameo ambaye pia ni Mwenyekiti wa bodi ya shule hiyo alisema kuwa madai ya wanafunzi hao yana ukweli ndani yake na kuahidi yeye na bodi kuyapatia ufumbuzi haraka, suala la mwalimu mkuu watamuondoa kwa kufuata taratibu na sheria kutokana na kuonekana hawezi kuongoza shule hiyo.

Hata hivyo wanafunzi hao walianza maandamano jana saa 5.30 asubuhi wakitoka eneo la shule hiyo iliyoko nje kidogo ya manispaa pasipo walinzi na walimu kujua wanakoelekea, ikiwa ni mara ya pili wanafunzi hao kudai haki zao, mara ya kwanza walifanya mgomo mwaka jana na mwaka huu wameamua kufanya maandamano ya amani.  

No comments:

Post a Comment