Kassim Mahege na
Rehema Maigala
SERIKALI itahakikisha inapambana na maharamia dhidi ya wanyamapori ikiwa
ni pamoja na watu wote wanaotoa fedha kwa lengo la kusaidia vitendo vya
kijangili, bila kujali nyadhifa zao wala madaraka waliyokuwa nayo nchini.
Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Utalii Lazaro
Nyalandu wakati alipotembelea katika Maonyesho ya Biashara ya Kimataifa
Sabasaba Jijini Dar es Salaam jana kuwa wizara yake itahakikisha inawakamata
Wakubwa wanaofadhili ujangili duniani kote. “Kupitia mfumo wa Air
Transport Infrastructure, kwa kushirikiana na Serikali ya watu wa Marekani,
tutawakamata vigogo wote duniani wanaodhamini Ujangili,”alisema Nyalandu.
Akifafanua zaidi alisema zamani maharamia
hao walikuwa wakishughulika zaidi na Pembe za ndovu na kuongeza kuwa sasa hivi
wamewageukia Simba ambapo inaaminika kuwa ukipata moyo wake utatajirika, jambo
ambalo sio sahihi.
Alisema Sekta ya Utalii ndio sekta
inayotoa ajira nyingi zaidi hivyo Serikali itahakikisha inawakamata maharamia
hao hata kama watatumia magari makubwa (Fuso) yenye namba za Serikali.
Alisema hivi sasa kuna ujangili wa
wanyamapori na kuongeza kuwa katika Mkoa wa Dar es Salaam wapo watu hao hivyo
watapambana nao usiku na mchana ili kuwatia mikononi mwa vyombo vya dola.
“Sekta ya utalii mwaka jana imechangia
asilimia 17 katika pato la Taifa na ndio sekta pekee inayoingiza pesa nyingi za
kigeni, hivyo hatuwezi kuwaachia maharamia watawale katika sekta hiyo,”alisema
Nyalandu.
Alisema mwaka jana idadi ya watalii
ilikuwa 1.1 milioni na kuongeza kuwa mwaka huu malengo yao ni kufikisha idadi
ya watalii milioni mbili.
Alisema anapenda kuwasihi Watanzania wenye
tabia hiyo kuacha mara moja kwani atakayefanya vitendo vya ujangili lazima
atakamatwa.
No comments:
Post a Comment