30 July 2013

NSSF KUKOPESHA WANACHAMA WAKE



Na Mashaka Mhando, Tanga
MFUKO wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), unaandaa utaratibu wa k uwa k o p e s h a wanachama wake sehemu ya michango yao wanayolipa kila mwezi ili kuwasaidia kuboresha maisha na kupambana na umaskini.

Sanjari na hilo, mfuko huo umewataka wananchi nchini kubadili mitizamo yao ya kuchangia harusi na sherehe mbalimbali za kijamii na badala yake wawekeze sehemu ya fedha wanazozipata, katika mifuko ya hifadhi ya jamii.
Akizungumza katika semina ya siku tatu kwa Jumuiya ya Wanawake nchini (UWT) inayofanyika jijini Tanga, Meneja wa NSSF Mkoa wa Tanga, Frank Maduga alisema kuwa mfuko huo unaandaa utaratibu utakaowawezesha wanachama kukopeshwa fedha kukidhi mahitaji yao.
"Wadhamini wa mfuko wanaandaa utaratibu ambao utawawezesha kukopa kile wanachochangia kila mwezi, hii itawasaidia wanachama wetu kuona ni namna gani wanaweza kupambana na umaskini," alisema Maduga.
Alisema wananchi hapa nchini lazima wafahamu maisha yamekuwa na changamoto nyingi hivyo suala la kuhifadhi fedha katika mifuko ya jamii ni suala la kisheria ambalo wanatakiwa walipe kipaumbele kwa ajili ya kuwasaidia hapo baadaye.
"Wananchi lazima waweke kipaumbele katika suala la akiba kwa maisha ya baadaye...Hii michango ya harusi wanayojali zaidi haina faida wajue maisha yamekuwa na changamoto nyingi kwa sasa ni bora wakajali na kuwekeza katika mifuko ya jamii," alisema Maduga.
Hata hivyo alikemea tabia ya jamii ya watu wa Mkoa wa Tanga kila inapofika wakati wa sikukuu na mwanzoni mwa mwaka, wanajitoa kuchangia katika mfuko huo na kuchukua fedha zao kwa ajili ya matuminzi ya wakati huo akieleza kwamba hayana faida.
Alisema ni vyema wananchi wakaendelea kuchangia kwa faida ya baadaye kuliko kuchangia kisha kuchukua fedha hizo kwa lengo la kujitoa akieleza kwamba matokeo yake, hawawezi kujiwekea akiba ya mbeleni.
Miongoni mwa wajumbe katika semina hiyo, Mbunge Viti Maalum Singida, Martha Mlata alisema mafunzo hayo yametolewa muda mwafaka kwani yameweza kuwajenga kisiasa.
Alisema kuwa watahakikisha wanakwenda kuhamasisha wanachama ili waone umuhimu wa kujiunga na mfuko huo, kuweza kupata mafao ya uzeeni sambamba na matibabu pindi wanapougua.

No comments:

Post a Comment