26 July 2013

MWENGE KUMULIKA MIRADI YA BIL 2/- TABORA




Na Allan Ntana, Tabora
MWENGE wa uhuru ulioanza mbio zake jana katika Manispaa ya Tabora umezindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya sh. bil. 2. Hayo yalibainishwa na Mkuu wa Wilaya ya Tabora, Suleiman Kumchaya wakati akitoa taarifa ya miradi itakayozinduliwa katika manispaa hiyo mbele ya Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru, Juma Ali Simai.

Akisoma taarifa hiyo, Kumchaya alisema jumla ya miradi kumi na moja ya maendeleo itazinduliwa na kuwekwa mawe ya msingi ili kuharakisha jitihada zake za kuwaondolea kero wananchi wote waishio katika manispaa hiyo sambamba na kuwaletea maendeleo yaliyokusudiwa.
"Ndugu zangu tumedhamiria kumaliza kero zote zinazowakabili wananchi wetu katika wilaya hii, na huu ni mwanzo tu, ni imani yangu kuwa jitihada zetu hizi zitafanikiwa kwa uweza wa mwenyezi Mungu kwani tumeanza vizuri kwa mshikamano wa hali ya juu sana, ninawaombeni sana wananchi mwendelee kutupa ushirikiano," alisema.
Miradi iliyozinduliwa jana katika mbio hizo ni nyumba ya watumishi wa kituo cha afya Itetemia, mradi uliogharimu kiasi cha sh. mil. 82.5, mradi wa kikundi cha vijana wajasiriamali chenye wanachama 48 ambacho kimewezeshwa mashine 2 za kufyatulia tofali za kufungamana (interlocking bricks) zenye thamani ya sh. 900,000 na jengo la utawala la shule ya sekondari Kanyenye lililogharimu sh.mil.83.5.
Miradi mingine ni uzinduzi wa barabara ya Swetu yenye urefu wa km 0.997 katika Kata ya Cheyo iliyojengwa kwa kiwango cha lami kwa gharama ya sh. mil.145.3, mradi wa kisima kirefu cha maji safi ya kunywa katika Kijiji cha Kakurungu Kata ya Uyui kilichogharimu sh. mil. 3.4 na ujenzi wa ghala la kuhifadhia mazao katika kijiji cha Kapunze Kata ya Ikomwa lililogharimu sh.mil. 54.
Miradi mingine ni uzinduzi wa SACCOS ya Chama cha Walimu katika Manispaa ya Tabora yenye wanachama 411 na mtaji wa sh. mil. 480, klabu ya wapinga rushwa katika shule ya sekondari Kariakoo yenye jumla ya wananchama 198 (wavulana 113 na wasichana 85), vikundi 7 vya akina mama wajasiriamali ambavyo vimekopeshwa jumla ya sh. mil. 20 na mradi wa hifadhi ya msitu wa asili Mguluko-Misha wenye ukubwa wa hekari 18 ukiwa na thamani ya sh.mil. 129.4

No comments:

Post a Comment