02 July 2013

MILIONI 30/- ZATUMIKA KUKARABATI VIWANDA KILIMANJARO


KITUO cha Maendeleo ya Viwanda mkoani Kilimanjaro (KIDT), kimekarabati Tanuru la kuchoma Insulator katika kituo kidogo cha Wilaya ya Same kwa zaidi ya sh milioni 30 lengo likiwa ni kuongeza uzalishaji wa bidhaa hizo ambazo zinauhitaji mkubwa hapa nchini na nchi jirani.
Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake Meneja Mkuu wa KIDT, Mhandisi Frank Elisa alisema pamoja na kukarabati tanuru hilo bado wanauhitaji wa matanuru mengine mawili ili kuweza kukabiliana na changamoto kubwa ya uhitaji wa bidhaa hizo hapa nchini.
Mhandisi Elisa alisema kukarabatiwa kwa tanuru hilo kumeongeza uzalishaji wa Insulator kutoka 10,000 zilizokuwa zikizalishwa mwanzo hadi kufikia insulator 25,000 hivyo kupunguza tatizo la uhitaji wa bidhaa hizo.

"KIDT tunakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo upungufu wa matanuru na tunaendelea kukkabiliana nazo ili kuhakikisha tunazalisha bidhaa nyingi ambazo zitatosheleza hapa nchini na Afrika Mashariki kwa ujumla," alisema.
Katika hatua nyingine meneja huyo aliishauri serikali kupitia wizara ya viwanda, kuvilinda viwanda vilivyopo katika maeneo mbalimbali hapa nchini na kuhakikisha vinafanya kazi kwa ufanisi, hatua ambayo itasaidia kuleta mabadiliko ya kimaendeleo na kukuza uchumi wa nchi.
Alisema kuna haja ya Serikali kuvilinda viwanda vichache vilivyopo na mabavyo vinafanya kazi na kuhakikisha inaviongezea mtaji ili kuweza kuleta mabadiliko ya kimaendeleo na kukuza uchumi kupitia sekta ya viwanda hapa nchini.
Pia alisema Serikali imeonekana kuvisahau viwanda; hali ambayo imesababisha viwanda vingi kujiendesha kwa fedha za wateja hivyo kujikuta vikifanya kazi kwa kusuasua na kushindwa kuchangia mabadiliko ya kimaendeleo na kukuza uchumi wa nchi kama ilivyokusudiwa.
"Tunaiomba serikali ivilinde viwanda vya ndani na kuviongezea mtaji, kwani kwa sasa sisi wenyewe tunajiendesha kwa fedha za wateja na wakichelewa kulipa tunashindwa kuendelea mbele," alisema.
Kwa upande wake msimamizi wa Kituo cha KIDT wilayani Same ambacho kinahusika na utengenezaji wa Insulator na vyombo vya udongo na jamii yake, Loveness Mhina alisema, hali ya uzalishaji wa Insulator kwa sasa ni mzuri ikilinganishwa na kipindi cha nyuma.
Alisema pamoja na uzalishaji kuwa mzuri bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo upungufu wa matanuru ya kuchoma insulator na Shirika la Umeme nchini TANESCO kuchelewa kulipa fedha mara baada ya kuchukua insulator.
"Bidhaa yenye soko kubwa sasa ni Insulator ambazo huchukuliwa kwa oda na TANESCO lakini TANESCO huchelewa kulipa fedha, hali hii husababisha tushindwe kuendelea mbele kutokana na kukosa fedha za kujiendesha," alisema.
Aidha, alisema ni vema serikali ikaangalia uwezekano wa kuwaongezea matanuru mengine mawili katika kituo hicho, hatua ambayo itawawezesha kuzalisha bidhaa nyingi zaidi na kufanikisha jitihada za Serikali za kukuza ajira hapa nchini.

 

No comments:

Post a Comment