30 July 2013

MIGOGORO YA ARDHI KUPATIWA UFUMBUZI



Na Mwajabu Kigaza, Kigoma
KUKITHIRI kwa migogoro ya ardhi katika Manispaa ya Kigoma Ujiji mkoani Kigoma inayosababishwa na baadhi ya viongozi wa Manispaa hiyo imekuwa chanzo cha wananchi kukatana mapanga wakati wa maziko katika eneo la Bushabani lililopo katika Kata ya Kibirizi mkoani hapa
. Katibu wa Chama cha NRA Taifa, Hamisi Kiswaga ameamua kulishughulikia tatizo hilo ambalo lina muda mrefu bila kupatiwa ufumbuzi katika kata hiyo ambapo zaidi ya maiti tano kwa nyakati tofauti zilizuiliwa kuzikwa katika eneo la maziko na hivyo kulazimika kuzika chini ya usimamizi wa polisi kutokana na mgogoro wa ardhi.
Kiswaga alisema kuwa, amekuwa akipokea malalamiko ya wakazi wa eneo hilo kuzuiliwa kuzika kwenye makaburi yaliyopo katika mtaa wa Bushabani kwa kipindi cha mwaka huu jambo ambalo linazua balaa ambapo makaburi hayo yalikuwa yakitumika tangu mwaka 1987.
Aidha aliitaka Idara ya Mipango miji kutatua mgogoro huo wa sehemu ya kuzikia ya maiti katika mtaa huo ili kuepusha maafa yanayoweza kujitokeza kutokana na baadhi ya wakazi kudai kuwa eneo hilo ni lao na kusababisha wakazi wa eneo hilo kuzika maiti zao kwa usimamizi wa askari polisi.
Wakizungumzia jambo hilo kwa nyakati tofauti, Mwenyekiti mstaafu wa mtaa wa Bushabani, Haruna Bakunda na Lulinda Mustafa walisema kuwa chanzo cha vurugu hizo ni Mama Senga na familia yake ambao wanadai eneo hilo ni lao walilorithi toka kwa marehemu baba yao ambaye alikuwa mtawala wa eneo hilo enzi za ukoloni.
"Kero hii imekuwa ya muda mrefu na malalamiko yamefikishwa katika uongozi wa Manispaa pamoja na polisi, lakini hakuna hatua zilizokuwa zikichukuliwa ndiyo tukaamua kuonana na viongozi wa NRA ili watupatie msaada wa kutatua kero hiyo ambapo mama huyo na watoto wake wamekuwa tishio katika eneo hilo.
"Hivi karibuni limetokea sakata la kichapo hadi mtu mmoja kalazwa katika Hospitali ya Maweni kisa ni kukataza kuzika katika eneo hilo la makaburi, hii ni kero tunataka kuwa huru katika mazishi na sio kusimamiwa na polisi," alisema Mwenyekiti huyo mstaafu.
Akitoa majibu katika kikao maalumu na viongozi wa Chama cha NRA, wakazi wa eneo la Bushabani, Meya, OCD mbele ya Kaimu Mkurugenzi, Naibu meya wa Manispaa hiyo, Yunusi Ruhomvya alisema kuwa kwa mujibu wa sheria eneo hilo lipo kwa lengo la maziko na kuwataka wananchi hao wawe wavumilivu ili wapatiwe majibu yaliyo sahihi kutoka kwa viongozi wa mipango miji watakapomaliza kikao chao.
"Keshokutwa mtapata majibu sahihi kuhusu eneo hili, ikiwa ni pamoja na kupata ramani ya eneo hilo na kuondoa kero hiyo ambayo imekuwa ya muda mrefu," alisema Meya huyo..

No comments:

Post a Comment