23 July 2013

MATUMIZI YA KADI KUPUNGUZA MIGOGORO YA ARDHI


Esther Macha
WAJIBU na majukumu ya Madiwani ndani ya Halmashauri nchini ni kuwahudumia wananchi ili wajiletee maendeleo na pia kulenga kumwezesha diwani kuwa na fikra na mitazamo chanya katika ushirikiano wake na jamii.Wajibu wake utampasa kuwa kiongozi mwenye mwenendo wa kimaadili, mtazamo wa kifikra kuhusu juhudi za kazi, uzalendo, kujitegemea, udumishaji wa mshikamano wa jamii na umoja wa kitaifa katika kuendeleza amani na utulivu.

Hata hivyo, sifa za uongozi kidemokrasia katika uhamasishaji na kujenga uwezo wa jamii na stadi muhimu za mawasiliano na usuluhishi wa migogoro zimeelezwa ili kumjengea diwani sifa, uwezo na uhalali katika kutimiza majukumu yake.


Suala la uwazi na uwajibikaji katika kutimiza mahitaji ya ibara ya 8 ya Katiba imezingatiwa kwa kuelezea mifumo na taratibu zilizopo na kuonyesha nafasi zake katika kukuza dhana ya Uwazi na uwajibikaji.

Ili kuweza kutimiza hayo hivi karibuni Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya ilifanya ziara ya kimafunzo wilayani Kilombero mkoani Morogoro lengo likiwa ni utekelezaji bajeti ya mwaka wa fedha 2012/13 kupitia mradi wa kuwajengea uwezo madiwani nchini.

Mafunzo hayo ni nyenzo muhimu kwa madiwani wote ili waweze kupata mafunzo ya kiutendaji pamoja na kupata uelewa juu ya miradi mbalimbali ya kimaendeleo katika kata zao.

Lengo kuu la ziara hiyo ni ukusanyaji wa mapato yatokanayo na mchele,utatuzi wa migogoro ya wakulima na wafugaji, uhifadhi wa mazingira misitu na vyanzo vya maji, kilimo uzalishaji wa mpunga.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali, Bw.Kenneth Ndingo anasema kuwa lengo la ziara hiyo ya kimafunzo ni kubadilishana uzoefu na wilaya hiyo ya Kilombero kwani historia ya mahusiano ya kilimo na hali ya hewa inafanana .

"Unajua wilaya hii inafanana vitu vingi sana na Wilaya yetu ya Mbarali hivyo tuliona ni vema kuja kujifunza huku tujue wenzetu wanafanyaje kuhusu migogoro ya wakulima na wafugaji na hata upatikanaji wa mapato kwenye kilimo cha mchele," anasema Bw. Ndingo.

Hata hivyo, hatua waliyoanza nayo madiwani ni kutaka kujua utatuzi wa migogoro katika Wilaya ya Kilombero kama uongozi wa halmashauri wanatatua vipi. Diwani wa kata ya Luhanga, Bw.Baraka Leteyo alitaka kujua operesheni ya kupunguza mifugo Kilombero na idadi inayotakiwa kubaki kama wanyama kazi na kujibiwa kuwa wanyama wanaotakiwa kubaki ni nane wanaruhusiwa kubaki kama wanyama kazi na si zaidi.

Diwani mwingine wa Kata ya Ruiwa Bw. Alex Mdimilaje anasema kuwa walichoweza kujifunza katika ziara hiyo ni pamoja na wafugaji wa eneo hilo kuunda umoja wao ambao unawasaidia kutatua kero zao.

Bw. Mdimilaje anasema kuwa umoja huo pia unawasaidia kubaini wafugaji wanaoingia kinyemela wanaotoka mikoa ya jirani kuvamia Wilaya ya Kilombero baada ya mikoa waliyotoka kuhamishwa kinguvu.

"Pia kupitia umoja wao wanaweza kukopesheka katika taasisi mbali mbali za kifedha hivyo ni vema na sisi wilaya yetu ya Mbarali tukafanya mazungumzo na wafugaji wetu ili nasi tuweze kuwa na vitu kama hivi." anasema Diwani huyo.

Akizungumzia utatuzi huo wa migogoro, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero, Bw.Daudi Ligazio anasema kuwa mbinu zinazotumika kukabiliana na migogoro ya wakulima na wafugaji ni kuweka alama za mifugo,upimaji wa ardhi ya malisho,wafugaji kuwekewa kadi maalumu ya utambuzi, jumla ya vijiji 71 vimepimwa na kuwekewa mpango wa matumizi bora ya ardhi kati ya hivyo vijiji 24 vimepimwa kwa ajili ya ufugaji.

Hata hivyo, anasema kuwa wilaya ya Kilombero katika utatuzi huo wa migogoro wilaya ilihamisha mifugo 202,752 kati ya mifugo 24,578 iliyohamishwa kwa shuruti,mifugo 53,168 iliuzwa minadani na jumla mifugo 125,000 ilitoroshwa kupitia njia za panya.

Kitu kingine ambacho waliweza kujifunza Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya Mbarali ni ukusanyaji wa mapato ambapo halmashauri ya Wilaya ya Kilombero inatumia watendaji wa kata katika ukusanyaji wa ushuru tofauti na Wilaya ya Mbarali ambapo inatumia mawakala kukusanya ushuru huo.

Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Bw. Ligazio anasema kuwa ili kuweza kuboresha ushuru huo halmashauri hutoa motisha kwa watendaji wa kata, pia halmashauri imeunda timu ya ufuatiliaji wa mapato ambayo wajumbe wake hubadilishwa mara kwa mara na mwenyekiti wake akiwa ni Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Bi.Azimina Mbilinyi.

Kwa upande wake mweka hazina wa halmashauri hiyo, Bw.Mbwana Msangi anasema kuwa ili kuboresha mapato, halmashauri inatengeneza vitabu vyake vya ushuru kutoka Mpigachapa Mkuu wa Serikali ili kupunguza wizi utokanao na vitabu bandia na kila tarehe 15 ya mwezi lazima wanahakiki vitabu.

Akizungumzia kuhusu wazabuni mweka hazina huyo anasema kuwa hawajaweza kuwapa wazabuni kazi ya ukusanyaji ushuru mpaka pale watakapojiridhisha kwa kutembelea wilaya zingine kujifunza.

"Mikoa na wilaya ambazo tumeweza kutembelea kujifunza ni Jiji la Mwanza, Shinyanga, mapato yetu ya ndani ni wanayokusanya watendaji ni bil.3 kwa mwaka na kwamba hadi kufikia Juni mwaka 2013 ushuru wa mazao, nafaka watakuwa wamekusanya sh. bil.1.4," anasema Bw. Msangi.

Hata hivyo, anasema kwa wale wanasiasa ambao wana tabia ya kuchochea wananchi kutolipa ushuru mbalimbali kuwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Wilaya huchukua hatua ikiwemo suala hilo kuingizwa kwenye vikao na kumwomba diwani wa eneo husika kuacha uchochezi huo mara moja.

Kwa upande wake Ofisa kilimo na Takwimu Wilaya ya Mbarali Bw.Vanscar Kulanga alitaka kujua kama halmashauri ya Kilombero inatoza ushuru kwa kuzingatia vipimo vya uzito au ukubwa na lumbesa wanadhibiti vipi.

Kwa upande wa mweka hazina Wilaya ya Kilombero anasema kuwa, halmashauri inapambana na rumbesa kwa kutoza adhabu ya malipo zaidi ya kwa kila mfanyabiashara anayebainika kujaza lumbesa na baada ya kulipa adhabu huwa wanaamriwa kujaza upya kwa kuzingatia magunia yenye ujazo wa kilo 100.

Kwa upande wake Kaimu Mk u r u g e n z i Mt e n d a j i wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali Bi.Tyatawelu Mongo alitaka kujua ada za wanafunzi wa sekondari zinakuwa chanzo cha mapato ya halmashauri.

Mweka hazina Wilaya ya Kilombero anasema kuwa rekodi zote zinaingizwa kwenye vitabu vya halmashauri na kuwasilishwa kwenye vikao ila fedha hizo huwa zinabaki katika shule husika kwa mwongozo wa TAMISEMI.

Ziara hiyo ya kimafunzo ya madiwani wa halmashauri ya Wilaya ya Mbarali Mkoani Mbeya ilikuwa ya siku tano ambayo lengo lake ni utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha wa 2012/13 kupitia mradi wa kujenga uwezo (Capacity Building Grant).

Hata hivyo, ziara hiyo iliongozwa na wakuu wa idara mbalimbali wa halmashauri hiyo ikiwemo fedha, kilimo, mazao, maliasili,mifugo pamoja na mipango miji.

No comments:

Post a Comment