05 July 2013

MATATANI KWA KUKUTWA NA MIHADARATI


 Na Said Hauni, Lindi
WAKAZI wawili wa mji mdogo wa Masoko, Wilaya ya Kilwa, mkoani Lindi wanashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kukutwa na dawa za kulevya aina ya heroine na bangi kete 35.
Kwa mujibu wa Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani humo, Renata Mzinga, wakazi hao wamekamatwa katika msako uliofanywa Juni 29, mwaka huu saa 3:30 usiku.

Mzinga aliwataja waliokamatwa kuwa ni Abdullah Abdallah (30) na Mohamedi Maulidi Meli (18), wote wakazi wa mji mdogo wa Masoko, Wilaya ya Kilwa.
Alisema Abdallah alikamatwa eneo la Mkapa Garden akiwa na dawa za kulevya aina ya heroine gram mbili na mabomba matatu ya sindano yaliyokuwa yakitumika kujidungia.
Pia alisema Maulidi alikamatwa maeneo ya Shule ya Sekondari ya Kilwa akiwa na kete 35 za bangi ambayo alikuwa akiitumia kwa biashara.
Mzinga ameliambia gazeti hili kwamba watuhumiwa wote wawili tayari wameshafikishwa katika Mahakama ya Wilaya hiyo ya Kilwa kujibu mashtaka yanayowakabili.
Kaimu kamanda huyo wa polisi aliwaomba wananchi kushirikiana na jeshi hilo katika kuwafichua watu wanaojihusisha na vitendo ambavyo kimsingi havileti maendeleo mazuri kwa jamii.

No comments:

Post a Comment