26 July 2013

MAREKANI YAIMWAGIA SIFA TTCL



SERIKALI ya Marekani kupitia ubalozi wake nchini umepongeza kazi nzuri iliyofanywa na Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) wakati wa ziara ya Rais wa nchi hiyo, Barack Obama, anaripoti Mwandishi Wetu.
Wakati wa ziara ya Rais Obama, TTCL ilipewa dhamana ya kusimamia mawasiliano tangu akifika kiongozi huyo hadi kuondoka. Baadhi ya maofisa kutoka ubalozi wa nchi hiyo hapa nchini wakiongozwa na afisa wa ubalozi huo, Jeff Shrader, walifika makao makuu ya kampuni hiyo Jumatano wiki hii ambapo walikutana na uongozi pamoja na wafanyakazi waliohakikisha kuwa suala zima la mawasiliano linakwenda vizuri na kwa ufanisi.

Mkuu wa Masoko na Mauzo wa TTCL, Peter Ngota, aliwaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kuwa kampuni hiyo imepata faraja kubwa kwa kupata mrejesho huo kutoka serikali ya Marekani.
“Tumepata faraja hii inaonesha uwezo wetu kitaaluma na ubora wa vifaa tulivyo navyo katika kutoa huduma za mawasiliano,” alisema.
Alisema TTCL ilipewa sifa hasa kutokana na utaalamu, uchapa kazi na weledi wa hali ya juu uliooneshwa na wafanyakazi wa kampuni hiyo kwa timu ya Wamarekani waliokuwa wanafanya nayo kazi.
Wafanyakazi na viongozi kadhaa wa TTCL walipewa zawadi mbalimbali kama njia ya kutambua mchango wao.
Ngota alisema kuwa kampuni hiyo itaendelea kufanya juhudi kuhakikisha kuwa inakuwa mtoa huduma bora wa kimataifa wa mawasiliano hapa nchini.
Ujumbe huo wa Wamarekani umeahidi kutoa vyeti vya kutambua mchango wa TTCL na wafanyakazi wake katika siku chache zijazo.
Kampuni hiyo ya simu inaendesha na kusimamia mkongo wa taifa wa mawasiliano kwa niaba ya Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia.

No comments:

Post a Comment