29 July 2013

MAKATIBU WA CCM WAKABIDHIWA RUNGU




Na Thomas Mtinge, Mbeya 
MAKATIBU wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ngazi ya wilaya na mikoa nchini, wameagizwa kuwafukuza makatibu wa jumuiya za chama hicho watakaohudhuria vikao vya Sekretarieti bila kuwa na ajenda za vikao hivyo.


Agizo hilo limetolewa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa ya CCM, Abdallah Bulembo, wakati akizungumza kwa nyakati tofauti na Wajumbe wa Halmashauri Kuu za CCM, Mabaraza ya Wazazi,UWT na UVCCM katika wilaya za Mbalali na Kyela juzi.Kwa mujibu wa Bulembo, kila mjumbe anayehudhuria vikao hivyo lazima awe na ajenda ya kuiwasilisha katika kikao husika ili iweze kujadiliwa kwa pamoja na kuipatia ufumbuzi.
"Vikao vya Sekretarieti si vya kukutana kwa ajili ya kunywa soda na kupika majungu, bali ni vikao vya kujadili mambo muhimu ya nchi na mustakabali wa chama," alisema na kuongeza;"Sasa kama kuna wajumbe waonadhani hivyo ni vikao vya kunywa soda na kupika majungu, basi wafukuzwe maana hawatufai wameshindwa kazi, hivyo mtoe nje ili akajipange tena wala huna haja ya kumuonea aibu wala kufanya naye kazi kwa mazoea," alisema Bulembo.
Alisema pamoja na mambo mengine, wajumbe hao wanatakiwa kujadili kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu pale inapowezekana."Katika vikao vyenu mnatakiwa kujadili mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na mafanikio ya utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya chama chetu na kero za wananchi," alisema.
Alisema baada ya kujadili ajenda hizo, viongozi hao kwa pamoja wanatakiwa kushuka chini na kufanya mikutano ya hadhara ya wananchi ili kuwaeleza mafanikio ya utekelezaji wa ilani hiyo na mikakati iliyopo ya kutatua kero zao ili kuepuka upotoshaji unaoweza kufanywa na vyama vya upinzani.
Bulembo alisema baadhi ya vyama hivyo vya upinzani vimekuwa vikiwarubuni wananchi kwamba CCM haijafanya maendeleo yoyote tangu kuingia kwake madarakani jambo ambalo alisema si kweli.
"Mwenye macho haambiwi tazama. Hakuna mwananchi asiyejua au kuona mazuri mengi yaliyofanywa na serikali ya CCM katika nchi hii. Wapinzani wanapita mitaani na kuwadanganya wananchi kwa kuiponda Serikali ya CCM hao wamefilisika kisiasa kutokana na kuwa na mawazo mgando kifikra.
Ili kuepuka propaganda hizo, nendeni kwa wananchi mkakisemee chama chenu kwa kufanya mikutano ya hadhara na kuelezea mafanikio yaliyofanywa, yaliyopo na yanayotarajiwa ili wawapuuze," alisema Bulembo.
Alisema bila kufanya hivyo wananchi hao wanaweza kuamini kila kitakachosemwa na wapinzani hao hata kama hakina ukweli.

No comments:

Post a Comment