Na Abdallah
Amiri, Igunga
KUNDI la watu 20
wanaodhaniwa majambazi wameteka basi la kampuni ya Mohamed Trans Ltd lililokuwa
likitokea jijini Dar es Salaam kwenda Bukoba katika tukio lililotokea katika
Kijiji cha Igogo Wilaya ya Igunga, mkoani Tabora.Kwa
mujibu wa taarifa za Jeshi la Polisi Wilaya ya Igunga, zilieleza kuwa baada ya
abiria wa basi hilo kufika eneo la Igogo walikuta majambazi hao wamepanga mawe
na magogo katikati ya barabara na ndipo dereva ililazimika kusimama.
Baada
ya kusimama majambazi hao walianza kulishambulia kwa mawe na kuamuru kondakta
wa basi hilo awashushe abiria, amri ambayo aliitekeleza.Habari
kutoka polisi zilieleza kuwa basi lililotekwa ni lenye namba T840 AVW lilikuwa
na abiria 60. Tukio hilo lilitokea juzi saa tano na robo usiku. Baada
ya basi hilo kutekwa basi jingine la kampuni ya Summry lenye namba T 620 BEW
lililokuwa likiendeshwa na Moses Tindua (40), mkazi wa jijini Dar es Salaam
ambapo lilikuwa limesindikizwa na askari wawili likitokea Bukoba kuelekea
Jijini Dar es Salaam lilifika eneo hilo na ndipo polisi walishuka na kuanza
kurusha risasi hewani na majambazi hao kufanikiwa kukimbia.
Askari waliofanikiwa
kuokoa abiria hao ni D 8105 PC Josephat na H 1476 PC Athumani wote wa Kituo cha
Polisi wilayani Igunga.Askari hao waliongeza
kuwa kutokana na mwanga wa gari majambazi waliweza kuwaona na kufanikiwa
kukimbia. Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Wilaya ya Igunga, Abeid Maige,
alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa hakuna abiria aliyeibiwa
wala kujeruhiwa.
Aliongeza kuwa jeshi la polisi linaendelea kuwasaka majambazi hao na
kuwataka wananchi kutoa ushirikiano ili waweze kuwakamata na kuwafikisha katika
vyombo vya sheria. Hilo ni tukio la pili ndani ya kipindi cha mwezi huu, ambapo
hivi karibuni majambazi 10 yakiwa na silaha za kivita yaliteka mabasi mawili
yaliyokuwa yakitoka Bukoba kwenda Dar es Salaam na Arusha kwenye pori la
Biharamulo.
No comments:
Post a Comment