30 July 2013

KILOMBERO WAFICHUA SIRI HATI SAFI



 Na Lilian Justice, Morogoro
HALMASHAURI ya Wilaya ya Kilombero imebainisha kuwa kuendelea kupata hati inayoridhisha katika ukaguzi wa mahesabu yake ni kutokana na kuwepo ushirikiano mzuri baina ya madiwani na watendaji wa halmashauri hiyo.

Hayo yalibainishwa jana na Kaimu Mkaguzi mkazi kutoka ofisi ya ukaguzi Mkoa wa Morogoro, Jacob Ndaki wakati akisoma taarifa ya ukaguzi katika halmashauri hiyo katika kikao cha baraza la madiwani ambapo alisema kuwa halmashauri hiyo imefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuonesha kwa vitendo juu ya uwazi na uwajibikaji wa pamoja kwani kwa mfululizo wa miaka mitatu imekuwa ikipata hati hiyo.
Ndaki alisema kuwa halmashauri hiyo inatakiwa kuendeleza juhudi hizo na kusimamia ipasavyo mapato na matumizi katika vijiji na kata zake zote ili utendaji kazi wake uweze kustawisha halmashauri hiyo, mkoa na Taifa kwa ujumla.
Aidha alifafanua kuwa katika kipindi cha mwaka 2011/2012 halmashauri hiyo imeonesha kuimarika katika kufunga na uainishaji wa taarifa zake zenye picha sahihi ya pato na matumizi na kuutaka uongozi kuelekeza nguvu katika kuboresha zaidi huduma.
Alisema katika ukaguzi huo masuala mbalimbali yalipewa msisitizo wa pekee katika taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali huku akiainisha baadhi ya changamoto ikiwemo ya kutorejeshwa hazina mishahara inayokadiriwa kufikia shilingi milioni 49.
Alisema nyingine ni asilimia 20 ya ruzuku ya vyanzo vilivyofutwa kutopelekwa vijijini mfano kati ya shilingi milioni 88 ni shilingi milioni 55 zimebainika kupelekwa vijijini huku shilingi milioni 33 zikiwa hazijapelekwa.
Hata hivyo Mkaguzi huyo alisema kuwa katika manunuzi mbalimbali shilingi milioni 22 zilihusika kati ya hizo kiasi cha shilingi milioni 14 ni manunuzi yaliyofanywa kwa njia ya masurufu huku taarifa ikionesha kuhakikiwa shilingi mil.4.6 wakati shilingi mil.17.8 zikionesha hesabu zisizoridhisha.  

No comments:

Post a Comment