30 July 2013

ASILIMIA 97 WENYE FISTULA HUNYANYAPALIWA NA JAMII



Na Mwajabu Kigaza, Kigoma
IMEBAINIKA kuwa asilimia 97 ya wanawake wenye ugonjwa wa fistula huachwa na waume zao pamoja na kunyanyapaliwa na jamii kutokana na kukutwa na tatizo hilo. Kauli hiyo imetolewa na Meneja wa hospitali ya CCBRT ya Dar es Salaam, Kaspar Mmuya wakati wa kikao maalumu kilichofanyika wilayani Kasulu kwa lengo la kugawa rasilimali kati ya Wilaya mpya ya Buhigwe na Wilaya Kongwe ya Kasulu mkoani Kigoma.

Mmuya alisema kuwa tatizo linalowakumba akinamama hao imekuwa kikwazo katika familia zao na jamii kwa ujumla kuwatenga kutokana na tatizo hilo linalotokana na uzazi. Aidha aliwataka viongozi wa kata,washirikiane na madiwani kuelimisha jamii ili iondokane na tabia hiyo ya unyanyapaa kwa akinamama hao pamoja na waume zao kushirikiana na akinamama hao kuwapatia matibabu.
Akitoa taarifa za utafiti uliofanywa na CCBRT kwa ushirikiano na utawala wa Hospitali ya Kabanga, Dkt. Alphonce Lutumo alisema kuwa asilimia 97 ya wanawake wameachika toka kwa waume zao na asilimia 95 ya watoto wanaozaliwa hupoteza maisha.
Dkt.Lutumo amesema kuwa, Januari 2013 hadi Julai wanawake sita walifanyiwa upasuaji katika Hospitali ya Kabanga wilayani Kasulu mkoani Kigoma ambapo hivi karibuni kutakuwa na kampeni ya fichua waathirika wa fistula wilayani Kibondo.
Aidha Mganga mkuu msaidizi Hospitali ya Kasulu, Dkt. Cosmas Buguzi aliipongeza Hospitali ya Kabanga kwa kushiriki vyema kwenye kampeni hiyo ambayo inatoa huduma mbalimbali za afya kwa wananchi waliopo katika Wilaya za Buhigwe,Kakonko,Kasulu, Kibondo, Kigoma na Uvinza mkoani Kigoma.

No comments:

Post a Comment