30 July 2013

JK AONYA UHAMIAJI KUHUSU WAHAMIAJI HARAMU



Na Theonestina Juma, Kagera
ULEGEVU wa maofisa wa Idara ya Uhamiaji nchini hasa maeneo ya mipakani umetajwa kuwa chanzo cha wahamiaji haramu kufikia zaidi ya 56,000 kutokana na kujua bei zao ndogo, jambo ambalo ni tishio na hatari kwa usalama wa nchi kwa miaka 50 ijayo. Kauli hiyo imetolewa na Rais Jakaya Kikwete, wakati wa majumuisho ya ziara yake ya siku sita mkoani hapa.

Alisema ulegevu wa maofisa wa idara ya uhamiaji haramu ya kutokuwa wafuatiliaji , wao ni chanzo na sehemu ya tatizo, kwani pindi watu hao wanapoingia hakuna anayewafuatilia na kuwauliza wameingiaje nchini, kibali kiko wapi, matokeo yake wanaingia nchini kwa kasi ya ajabu. Alisema maofisa hao wanatakiwa kusimamia kikamilifu utambuzi wa watu wasio raia na kufuatilia vitabu walivyopeleka maeneo ya vijijini, kata na tarafa.
"Kuna watu wanaishi nchi hii kwa kibali cha mtendaji wa kijiji, ofisa mtendaji wa kata, kwa kuhongwa ng'ombe wawili, lakini kwa afisa uhamiaji makini lazima amfuatilie yule mtu na kumuuliza umeingiaje humu, akimwonesha kibali cha mtendaji awakamate na kuwapeleka wote mahakamani kwani wanakuwa wameingilia kazi ya Idara ya Uhamiaji," alisema.
Alisema katika suala hili la wahamiaji haramu, msako sio jibu akiingia nchini aondoke kwani Serikali haiwezi kupata sh. milioni 800 kwa ajili ya kushughulikia tatizo hilo. Pia Rais Kikwete alisema kuwa chanzo cha kuharibika kwa usalama kwa upande wa Kagera ni kutokana na kuingia kwa wakimbizi nchini ambapo mwaka 1963 walikuwa ni wa aina nyingine ambapo tena walioingia mwaka 1993 waliingia nchini na bunduki zao.

No comments:

Post a Comment