Na Elizabeth Mayemba
MSHAMBULIAJI wa Yanga, Hamis Kiiza
ambaye amekuwa akiidengulia klabu hiyo kuongeza mkataba mpya jana jioni
alitarajiwa kutua nchini akitokea kwao Uganda kwa ajili ya kuja kumalizana
na klabu hiyo.
Awali Kiiza
alikuja nchini kwa lengo la kumalizana na uongozi huo, lakini inadaiwa kuwa
ilishindikana na hivyo akarejea tena Uganda.
Hata hivyo
uongozi wa klabu hiyo, ulisema usingeweza kuzungumza lolote kuhusiana na
mchezaji huyo mpaka pale mtu wake wa karibu ambaye ndiye aliyemleta, Mjumbe wa
Kamati ya Utendaji wa klabu hiyo, Mussa Katabalo aliyekuwa Ulaya kikazi, arejee
na yeye ndiye atakuwa mtu wa mwisho na hatima ya mchezaji huyo itajulikana.
Akizungumza na
gazeti hili jana mmoja wa marafiki zake wa karibu na Kiiza, alisema baada ya
Katabalo kutua nchini mchezaji huyo jana alitarajiwa kuwasili Dar
es Salaam jioni akitokea kwao Uganda.
"Jamaa
anakuja kumalizana na Yanga kwani, Katabalo ameshatua nchini mapema wiki hii,
hivyo atazungumza na Kiiza na hatima yake itajulikana kama
ataendelea kuichezea timu hiyo au la," alisema.
Rafiki huyo wa karibu na Kiiza alisema,
mchezaji huyo anaipenda Yanga lakini kikubwa anachotaka ni kukamilishiwa
matakwa yake, ili aweze kuitumikia klabu hiyo kwa msimu ujao wa Ligi Kuu
Tanzania Bara na michuano ya kimataifa.
Kiiza alimaliza mkataba wake na Yanga,
hivyo akataka aboreshewe mshahara pamoja na fedha za usajili, lakini klabu hiyo
ya Jangwani ikasema kuwa haiwezi kumlipa kiasi hicho cha fedha.
Mshambuliaji huyo alisema uwezo wake
bado ni mkubwa, hivyo anashangaa ni kwanini uongozi wake unashindwa kufanya
vile anavyotaka yeye kwa kuwa bado ana mapenzi mema na klabu hiyo.
Endapo Yanga itamsajili Kiiza anaweza
kuigharimu zaidi ya sh. milioni 100, ambapo alitaka dola za Marekani 45,000 za
usajili, nyumba ya sh.milioni 8.
Pia alitaka gari la sh. milioni 10 pamoja na dola za
Marekani 3,500 kwa ajili ya mshahara wake kila mwezi. Lakini baadaye akatoa
punguzo katika fedha za usajili na kutaka alipwe dola za Marekani 40,000.
No comments:
Post a Comment