25 July 2013

SHERIA NDOGO KUWABANA WACHAFUZI MAZINGIRA



 Na Jovither Kaijage, Ukerewe
HALMASHAURI ya Wilaya ya Ukerewe Mwanza inakamilisha mchakato wa sheria ndogo ya usafi wa mazingira ili kukabiliana na tatizo hilo.Ofisa afya na mazingira wa halmashauri ya wilaya hiyo, Joseph Bulugu amesema hayo baada kushiriki shughuli ya usafi wa mazingira ambayo Jumatano ya wiki hii imefanyika katika mtaa wa Mdoe mjini Nansio.

Akizungumza na wakazi wa mtaa huo alisema mbali ya faini ya papo kwa papo ya sh. 10,000 pia sheria hiyo inahusisha mambo mengine ikiwemo tozo ya sh. 4,800 kwa mwaka kwa kila kaya.Adhabu ya sh. 10,000 itatozwa kwa mtu yeyote atakayetupa uchafu wa aina yoyote ovyo huku sheria ya tozo za gharama za huduma zikitofautiana kutoka kaya hadi taasisi na miradi binafsi ya biashara kama vituo binafsi vya afya na shule, baa, nyumba za kulala wageni na maduka.
Sheria hiyo inayotarajiwa kuwasilishwa katika baraza lijalo la madiwani inaonesha viwango vya tozo kwa mwaka vitakuwa kati ya sh. 4,800 hadi 100,000 fedha ambayo zikikusanywa zitatumika kuendesha gharama za usafi wa mazingira katika mji wa Nansio.
Hata hivyo Bulugu alisema sheria hiyo baada ya kupitishwa na baraza la madiwani itapelekwa kwa waziri mwenye dhamana kabla ya kurejeshwa ili itumike kusimamia usafi wa mazingira katika wilaya hiyo.
Awali ilipendekezwa katika sheria hiyo itozwe adhabu ya papo hapo ya sh. 50,000 kwa anayetupa uchafu ovyo kabla ya Mkuu wa wilaya hiyo, Mery Tesha kushauri kiwango hicho kipunguzwe hadi sh. 10,000 ili sheria hiyo itekelezwe kwa urahisi
Tesha alisema kulingana na hali ya kipato cha wananchi walio wengi ni duni hivyo kama faini itakuwa kubwa haitatekelezeka na kusababisha walio wengi kushtakiwa mahakamani.


No comments:

Post a Comment