15 May 2013

Watu 16,000 wanatumia ARVs, Amana

Na Heri Shaaban


 WATOTO 5,000 wenye umri wa miaka 10 kushuka chini, wanatumia dawa za kupunguza makali ya virusi vya UKIMWI (ARVs), katika Hospitali ya Amana, Dar es Salaam.
Mbali ya watoto hao, watu wazima 11,000 nao wameanza kutumia dawa hizo katika kliniki iliyopo hospitalini hapo.
 Daktari wa Kitengo cha Kuratibu Wagonjwa wa UKIMWI, Shani Mwaruka, aliyasema hayo wakati kamati ya kudhibiti ugonjwa huo Manispaa ya Ilala, ilipofanya ziara katika hospitali hiyo.
Alisema kwa siku kliniki hiyo uhudumia wagonjwa 250 hadi
300 ambao wanatoka kwenye maeneo mbalimbali na kudai kuwa, changamoto waliyonayo ni baadhi ya wagonjwa kutokubaliana na hali waliyonayo pamoja na uchache wa vitendea kazi.
“Watu wengi hawakubaliani na hali waliyonayo, baba anapokuja kupima afya yake anamficha mkewe na kuanza kutumia dawa peke yake na wanawake pia hivyo hivyo,” alisema Dkt. Mwaruka.
Aliongeza kuwa, kitengo hicho kinafanya jitihada za kuhakikisha wazazi wanawaeleza watoto wanaotumia dawa hizo wanapokua.
Kwa upande wake, Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Bw. Said Kitambuliyo, alisema lengo lao ni kutembelea mitandao yote na asasi za watu waishio na ugonjwa huo, kusikiliza changamoto walizonazo na kuangalia kazi wanazofanya.

No comments:

Post a Comment