15 May 2013

Lori lapinduka, laua 3 Mbeya

Na Esther Macha, Mbeya


 VIBARUA watatu wa kampuni inayojenga barabara ya China Communication and Construction Company (CCCC), mkoani Mbeya, wamefariki dunia kwenye ajali ya gari baada ya lori walilopanda likitoka kuchukua kifusi kupinduka.
Kamanda wa Polisi mkoani humo, Diwani Athuman, alisema tukio hilo limetokea jana saa sita mchana katika eneo la Iganzo, maarufu kama Mwisho wa Lami, barabara ya Mbeya-Chunya.
Alisema gari hilo lenye namba T 405 BWA aina ya
Zhongji mali ya kampuni hiyo, lilikuwa likitoka kuchukua kifusi katika eneo la Kawetele, ambapo dereva aliyesababisha vifo hivyo jina lake halikufahamika mara moja baada ya kukimbia.
Aliongeza kuwa, lori hilo lilipinduka baada ya dereva huyo kushindwa kulimudu kutokana na mwendo kasi katika eneo lenye kona na mteremko mkali.
Hata hivyo Kamanda Athuman alisema marehemu wote ambao miili yao imehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa mkoani humo, bado hawajatambuliwa.
Alisema katika ajali hiyo kulikuwa na majeruhi watano kati yao watatu walitibiwa hospitali na kuruhusiwa, wawili wamelazwa katika hospitali hiyo.
Aliwataja majeruhi wanaoendelea na matibabu kuwa ni msimamizi wa vibarua hao raia wa China, Don Fung Cheng (38), aliyejeruhiwa kichwani, pamoja na mtu mwingine ambaye hajafahamika jina kutokana na hali yake kuwa mbaya.
Waliotibiwa na kuruhusiwa ni Ayoub Samson (25), Jelicko Apton(18) na Natifa Ngole (23), wote wakazi wa Mkoa huo.

No comments:

Post a Comment