30 May 2013

Wakulima Bumbuli wang'oa chai, wapanda mahindi

Na Yusuph Mussa, Lushoto

MGOGORO wa wakulima wa chai, Chama cha Wakulima wa Chai Usambar a (UTEGA) na mwekezajiShadadMullah umeingia sura mpya baada ya wakulima hao kuamua kung’oa zao la chai na kupanda mahindi. Wakulima hao wanadai kilimo cha chai kimekuwa ni sawa na biashara haramu kwao. Hayo waliyabainisha kwa nyakati tofauti juzi nje ya uzio wa Kiwanda cha Chai Mponde kilichopo Halmashauri ya Bumbuli wilayani Lushoto wakati wakizungumza na mwandishi wa habari hizi. Walisema, wao kulima chai na kuiuza kwenye kiwanda bila kulipwa vizuri wakati ni wabia ni sawa na kero. “Mwandishi angalia upande ule tumeamua kung’oa chai na kupanda mahindi, tumeona kwetu hii ni biashara haramu, kwani hatufaidiki nayo pamoja na kwamba sisi ni wabia kupitia Chama wa
Wakulima cha UTEGA,” alisema Juma Sheshe. Naye mkulima Mustafa Soa alisema, wamenyanyasika kwa miaka 13 tangu UTEGA waingie ubia na mwekezaji huyo huku wakiwa hawajui mapato na matumizi wala hisa zao kwenye kiwanda hicho ni kiasi gani. Aidha, Sauli Makasi alisema wameanza kuzalisha kwa faida kwenye kiwanda hicho miaka nane iliyopita lakini hakuna chochote wanachopata huku wakijiuliza wao wapo ubia kati ya wakulima na mwekezaji, lakini mbona kuna mashirika yanaundwa katikati yake. “Sisi tumeingia ubia na mwekezaji, lakini kuna mashirika yameundwa katikati yetu kutunyonya, mfano kuna Lushoto Tea Estate na pia kuna Mponde Tea Estate haya yanafanya kazi gani,” alisema Makasi. Hata hivyo wakulima hao walikanusha kufanya fujo kwenye kiwanda hicho kama ilivyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari kupitia Jeshi la Polisi. Walidai sababu za kutokufanya fujo katika kiwanda hicho wana hisa kwenye zao na wameamua kukilinda usiku na mchana kusitokee kitu ama kuingia kiwandani hapo. “Tunalinda mali zetu na ndiyo maana tupo hapa. Angalia kiwanda kipo salama na hakuna kitu kilichoharibiwa ndani ya kiwanda hiki,” alisema Almas Shemshami. Mmoja wa mgambo wanaolinda kiwanda hicho, Festo Ngoda alikiri kutoharibiwa mali yoyote kiwandani humo ila yeye alipigwa na ubapa wa panga baada ya kuonekana yupo nyuma ya kiwanda hicho akihisiwa kama anataka kutoroka. Akizungumza na waandishi wa habari mwekezaji Mullah alisema, ndani ya mgogoro huo kuna mambo ya kisiasa huku akitupa lawama kwa Mbunge wa Jimbo la Bumbuli, January Makamba kuwa hajawaonesha ushirikiano katika kumaliza kero na changamoto za wakulima wa chai. “Tangu mwaka 2008 tumekuwa na matatizo ya kukiendesha kiwanda, baada ya msitu wetu wa miti wa Sakare wilayani Korogwe kwa ajili ya kuni za kukausha chai kuzuiwa tusivune na sasa wakulima wanadai hawataleta chai. “Suala hili limechangiwa na Mbunge January kushindwa kutoa ushirikiano kwetu, lakini tunaamini angekuwa karibu yetu isingefikia hapa, lakini sisi tunasema tupo pale kama wabia. Ni baada ya Serikali kubinafsisha kiwanda mwaka 1998 na sisi kuingia ubia na wakulima,” alisema Mullah. Akizungumza kwa simu na mwandishi wa habari hizi akiwa Dodoma, Makamba alisema sio kweli kuwa ameshindwa kutoa ushirikiano bali amekwishafanya vikao na mwekezaji huyo kupitia familia yake ikiwemo kuwaita ofisini kwake Dar es Salaam ili kujua mustakabali wa chai na wakulima wao. “Nimekaa na baba yake mzee Mullah na kaka yake Yusuph zaidi ya mara tatu. Tumefanya makubaliano kadhaa kuhusu namna ya kutatua tatizo, lakini hawakutekeleza. Pia tulikaa ofisini kwangu na mzee Mullah, Yusuph na Mkurugenzi wa Bodi ya Chai nchini (Assenga) hakuna ufumbuzi uliopatikana. “Kuna kikundi kinaitwa Ushirika walikuwa hawapeleki majani pale na kiwanda kikawa hakipati majani, Yusuph akaniambia nikawashawishi Ushirika wapeleke majani, wakaanza kupeleka hadi leo. Anataka ushirikiano gani,” alihoji Makamba. Hata hivyo kiwanda hicho kimeingia kwenye mgogoro baada ya mkutano uliofanyika Mei 26, mwaka huu kati ya wakulima na Makamba ambapo wakulima walitoa azimio la kutokiuzia malighafi kiwanda hicho baaada ya kuona hawapati faida.

No comments:

Post a Comment